Kuna watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaendelea kuteseka kiroho na kimwili.
Hawa ni watu ambao wanakumbana na vita, njaa, umaskini, magonjwa pamoja na majanga
asilia. Myumbo wa uchumi kimataifa umepelekea watu wengi kukosa fursa za ajira, kukosa
uwezo wa kuhudumia familia zao na pengine hata kukata tamaa.
Yote haya ni
mahangaiko yanayogusa maelfu ya watu duniani! Kuna watu pia wanaendelea kunyanyaswa
na kudhulumiwa kutokana na misimamo mikali ya kiimani; watu wanateseka kutokana na
kinzani na misigano ya kisiasa, kiuchumi na kijamii.
Baba Mtakatifu Francisko
katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii, anamwomba Mwenyezi Mungu
aweze kuwafariji watu wote wanaoteseka hususan wagonjwa, watu wenye shida na mahangaiko
mbali mbali pamoja na watu wasiokuwa na fursa za ajira.