Wanajeshi wasaliti watiwa pingu kwa kushirikiana na Boko Haram nchini Nigeria
Viongozi wa Jeshi la Nigeria wamewatia pingu baadhi ya askari wa majeshi ya ulinzi
na usalama nchini Nigeria kwa kushirikiana na Kikundi cha kigaidi cha Boko Haramu
katika kuendesha mashambulizi kadhaa nchini humo katika kipindi cha miaka mitano sasa.
Usaliti huu umepelekea maelfu ya wananchi wasiokuwa na hatia kuuwawa kinyama sanjari
na uharibifu mkubwa wa miundo mbinu.
Taarifa inasema kwamba, wanajeshi hao
walikuwa wamejipenyeza katika vikosi maalum vilivyokuwa vinaendesha operesheni tokomeza
Boko Haram nchini Nigeria, zoezi ambalo hadi wakati huu halijapata mafanikio ya kuridhisha,
kiasi hata cha kuzidiwa nguvu na Boko Haram. Askari hawa wamekuwa wakitoa taarifa
za siri kwa Boko Haram, kiasi hata cha kusababisha maafa makubwa kwa wanajeshi wenzao,
hali ambayo imepelekea hata wanajeshi wenyewe kutoaminiana kwa kiasi kikubwa.
Taarifa
ya kijeshi inasema kwamba, baada ya uchunguzi wa kina, askari waliokuwa wanalisaliti
Jeshi walibainika. Hawa ni wanajeshi ambao walikuwa wanashirikiana kwa karibu zaidi
na wakuu wa vikosi maalum bya oporesheni dhidi ya Boko Haram.