2014-10-13 09:44:58

Mwalimu Nyerere awe ni mfano wa kuigwa katika kusimamia: haki, amani na mshikamano wa kitaifa!


Askofu mkuu Josephat Louis Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha, Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Tanzania inapoadhimisha kumbu kumbu ya kifo cha Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tarehe 14 Oktoba, anawaalika watanzania kumuenzi Mwalimu kwa kujikita katika misingi ya haki, amani, umoja, mshikamano, utu, heshima na mafao ya wengi. RealAudioMP3

Askofu mkuu Lebulu anasema, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ni kiongozi aliyejipambanua kwa moyo wa uzalendo, akasimamia haki, amani na mshikamano wa kitaifa. Ni kiongozi aliyewajali watu wake kiasi hata cha kuyasadaka maisha yake kwa ajili ya ustawi wa Watanzania na Afrika katika ujumla wake. Kwa Mwalimu uongozi kilikuwa ni kielelezo cha huduma.

Askofu mkuu Lebulu anawataka watanzania kujibidisha zaidi katika kushughulikia masuala nyeti na tete yanayowagusa watanzania katika ujumla wao, kwa kutambua kwamba, kila mtu anawajibika mbele ya Mungu, kwa jinsi gani anavyojitoa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watanzania wengi, kwa kuweka misingi thabiti ya mustakabali wa taifa katika masuala ya haki na amani; umoja na mshikamano wa kitaifa, ili kujenga taifa linalojipambanua katika Jamii ya kimataifa kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Askofu mkuu Lebulu anakiri wazi kwamba, katika mchakato wa kutunga Katiba Mpya ya Tanzania, nchi imetikiswa katika msingi wake wa umoja na mshikamano wa kitaifa. Lakini watanzania wanapaswa kutambua kwamba, kipaumbele cha kwanza hakina budi kutolewa kwa ajili ya utu na heshima ya binadamu, mafao na maendeleo ya watanzania wote. Mwalimu Julius Kambarage Nyerere awe ni mfano wa kuigwa katika kusimamia misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.