2014-10-10 15:42:57

Zanzibar-Kejeli na mateso viliwapa imani zaidi kwa Msalaba wa Yesu


Mateso na kejeli za kidini zinazo fanyiwa dhidi ya Wakristo katika visiwa vya Zanzibar, matukio hayo yamekuwa kichecheo kwa Wakristo, kuimarisha zaidi imani yao na kuona fahari zaidi Msalaba wa Kristo.Ni ushuhuda ulioonekana katika Parokia ya Mtakatifu Malaika Mkuu Mikaeli, wakati wa sherehe ya watoto 104, kupokea kwa mara ya kwanza Ekaristi Takatifu.

Askofu wa Jimbo Katoliki Zanzibar, Mhashamu Augustino Shao ameeleza kuwa, imani ya Kikristo inapigwa vita, makanisa yalichomwa na wengine kuumizwa,lakini hawajachukua hatua za kulipiza kisasi kwa kuwa kulipa kisasi, si imani ya Kanisa Katoliki.

Alieleza katika homilia yake, wakati akitoa Sakramenti ya Komunio ya Kwanza kwa watoto 104 katika Parokia ya Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu, jimboni Zanzibar, wakati huohuo waamini wa parokia hiyo walipokuwa wanasherehekea sikukuu ya somo wa parokia hiyo Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu.

Askofu Shao alikumbusha, miaka miwili iliyopita Kanisa hilo, lilichomwa moto na watu wenye misimamo mikali ya kiimani, lakini leo hii limesimama upya na watu wa Mungu wanapata nafasi ya kusali na kuongea na Mungu wao. Ijapokuwa lilichomwa waamini hawakukata tamaa, wameendelea kushikana mikono na kutembea pamoja kwa upendo. Vijana wengi wanapata sakramenti mbalimbali za Kanisa kama watoto hao 104, walio pokea Komunio ya Kwanza leo.

Aliendelea kuwasifu Wakristo hao kwa kushika mafundisho ya Kanisa,akisema, licha ya dhuluma wanazo fanyiwa kama Wakristo, hakuna mtu aliyeenda kulipiza kisasi na wala hawana mpango wa kulipiza kisasi, kwani ni kinyume na imani ya Kanisa Katoliki na mafundisho yake. Aliwatia moyo Wakristo Jimboni mwake akisema, "Kazi yetu ni kusali na kuendeleza umoja wetu kwani wakati wa matatizo umoja ndio unaosaidia kutatua matatizo mbalimbali. Tungetengana Kanisa hili lililokuwa limechomwa hapa Mpendae lisingesimama tena.”

Aliendelea kuwaasa kwamba, uovu hata siku moja hauwezi kutenda wema, waliowachomea Kanisa hilo mwaka 2012 sasa wanaona aibu na kushangalia ukuu wa Mungu.Wakati wa mateso na kejeli za kidini, waliweza kupata nguvu zaidi za kuijenga imani katika Msalaba wa Kristo Msulubiwa.

Amewaasa waamini kuendelea kuwa chombo cha amani katika jamii, kuionyesha nguvu ya mwanga wa Mungu, kupitia shuhuda za kweli katika maisha na hasa wakati wa kupambana na changamoto.

“Waamini umoja mliyouonesha wakati wa tabu muuneshe pia wakati wa raha. Kwa kujenga hili Kanisa upya, mlijinyima mengi hadi leo, hiyo ndiyo sadaka yenye nguvu na Kristo awatie nguvu,” ameeleza.

Hata hivyo amesema kuwa, ijapokuwa Kanisa halina malumbano na kazi yake ni kusali kwa ajili ya jamii, halitasita kukemea na kuonya pale ambapo linaona makosa na upotoshaji unafanyika kwani kusema ukweli ni wajibu wa Kanisa.

Na akatoa wito kwa waamini kuwaombea viongozi wa serikali, ili waondokane na ubinafsi hasa wakati huu wa majadiliano ya mchakato wa Katiba Mpya. Tuwaombee walete katiba inayojenga umoja na amani kati ya jamii yetu,” ameeleza.

Na aliwaonya waamini wanaopigana na kufarakana kwa ajili ya mchakato wa katiba kwamba hata kama kuna vipengere visivyo wapendeza au kuwa vya kweli na visivyo jenga haki, umoja na mshikamano, wawe watulivu wasubiri kukataa wakati wa upigaji kura.

Katika sherehe hizo vijana waliopata Sakramenti ya Komuniuo ya Kwanza katika parokia hiyo ni 104, wakiwepo baadhi ya watoto kutoka familia za kiislamu na kiluteri waliotolewa na wazazi wao kwa nia moja waingie katika imani ya Kanisa Katoliki.

Paroko wa Parokia hiyo Padri Mushi ameeleza kwamba hata yeye alishangazwa na mtoto mmoja wa Kiislamu aliyekuja kwake akitaka kubatizwa na kupokea Ekaristi ya kwanza.

“Nilikataa kwa mara kadhaa lakini wazazi wa watoto hawa walikuja wakisema, Padri watoto hawa tumeamua wenyewe wawe wakristo katika Kanisa Katoliki. Tumewatoa kwa Kanisa ingawa sisi ni waislamu. Basi taratibu nyingine za Kanisa zikafuata hadi leo hii wamepata Sakramenti ya Kumunio ya Kwanza,” ameeleza Padri Mushi.








All the contents on this site are copyrighted ©.