2014-10-07 16:15:16

Tafakari ya Neno la Mungu Dominika ya 27 ya Mwaka A, 5 Oktoba.


Mpendwa, Karibu katika tafakari ya Neno la Mungu, tugange yaliyomo katika neno hilo tukiongozwa na nabii Isaya anayetupa ujumbe wa Mungu kwa kielelezo cha shamba la mzabibu, na kama kawaida Mtume Paulo akiwaandikia Wafilipi anatukumbusha wajibu wa kuhangaikia zaidi maisha ya sala iliyo njia ya mahusiano na Mungu zaidi ya mambo mengine ambayo kadiri ya mwinjili Mathayo yaliwafanya Waisraeli wapoteze sifa ya kuwa taifa teule, sifa ya kuwa shamba la mzabibu, na badala yake Mungu anaanzisha Kanisa, ambalo ni shamba jipya la mzabibu.

Nabii Isaya anasimulia juu ya shamba la mzabibu jinsi Bwana alivyo weka bidii na fedha kwa ajili ya kulitunza. Anatarajia matunda mazuri ya zabibu yenye kuleta faida. Lakini badala yake mizabibu inazaa matunda mwitu! Wale majirani wa Bwana huyu, walioona uwajibikaji wake, na sifa alizokuwa akitoa kwa shamba lake la mzabibu, wanaanza kumcheka na kinachofuata ni maskitiko kwake. Akiwa na ghadhabu kubwa anaamua kuondoa wigo aliokuwa amezungushia shamba hilo.

Mpendwa, huyu Bwana ni nani na shamba ni nini? Kwa hakika huyu bwana ni Mungu na shamba ndiyo taifa la Israeli ambalo Mungu alilipenda, alilolizungushia wigo toka utumwani Misri lakini badala yake limemwacha Bwana na kuzaa matunda mwitu! Mpendwa, hivi leo, sote tu shamba la mzabibu, tumetengenezwa vema kwa njia ya ubatizo, kipaimara na Ekaristi Takatifu ndizo neema zake, lakini oneni magugu ya kila aina ndiyo dhambi, magugu yanayoota katika ulimwengu huu juu ya migongo ya wabatizwa. Hakika tunajiuliza je bado ni shamba la mizabibu? Nabii Isaya anatualika kuacha kuzalisha magugu zaidi, vinginevyo wigo uliozungushiwa shamba hili ndizo neema zake utaondolewa kwetu na uzuri wa shamba utapotea ndiyo kupoteza uzima wa wana wa Mungu.

Mwinjili Mathayo anakazia ujumbe huo unaoelezwa kwa picha ya shamba la mzabibu, akisema Bwana mmoja mkulima wa mizabibu amewapangisha wakulima ambao anatarajia wampe malipo yanayomstahili baada ya mavuno. Lakini badala ya kumpa mastahili yake wanawaua watumishi ambao aliwatuma wakusanye malipo hayo. Tena mbaya zaidi wanamwua mtoto wa mwenye shamba ambaye alitarajiwa kuheshimiwa na kuogopwa na watumishi. Jambo hili ni kielelezo cha kukataliwa kwa manabii na hatimaye Mwana wa Mungu, Masiya mkombozi. Ni mlima wa kiburi cha mwanadamu.

Mpendwa mwana wa Mungu, jambo hili halikuwa la kawaida na hata hivi leo linatushangaza kwa Waisraeli kumkataa Masiya. Tena, jambo hili linaonekana kuwa mbali lakini li karibu kabisa nasi na pengine ndani ya moyo wangu. Namkataa mtoto wa mwenye shamba kwa maana ya matendo yangu mabaya, kwa maana ya kutojali kwangu katika kuwaheshimu wengine, tofauti na lile agizo la Mwana anayesisitiza kupendana kama alivyotupenda sisi. Nimeacha watoto wangu wanataabika kwa kukosa mahitaji ya msingi au hata nimeshindwa kuwajenga katika tabia njema. Namkataa Mwana kwa kupokea kipaimara kama mtindo wa mavazi ambayo huja kwa muda tu na kisha kupita! Nakazia jambo hili na hasa mijini, watoto kadhaa baada ya kupata kipaimara ndiyo mwisho wa kufika kanisani. Kwa bahati, mmoja akifunga ndoa ndipo tutakutana na baada ya hilo sijui tutakutana naye wapi!

Lipo jambo jingine ambalo ningependa kukukumbusha tu ili ulitafakari, nalo ni thamani ya Misa takatifu. Yafaa kuheshimu kina, Misa takatifu katika maisha yako hata kama wengine watakosa heshima mbele ya Misa takatifu. Kumbuka ni sadaka ya Kristu, ni sadaka ya msalabani anapojitoa kwa ajili ya ukombozi wako. Hata unapokwenda kuomba Misa uwe makini, maana mara kadhaa utasikia baadhi ya waamini wakisema Misa shilingi ngapi! Au nirudishie chenji! Kumbuka Misa huwezi kuinunua na pia unapotoa sadaka, mkono wako wa kuume usijue mkono wa kushoto umetoa nini. Wengine huthubutu kusema Misa ni yangu, hapana, ni zawadi ya Kristu kwa ajili ya wote. Kumbe epuka mambo ya chenji na umiliki wa Misa Takatifu. Vitu hivi vyaweza kuonekana ni vya kawaida lakini polepole vinamengenyua adili katika maisha ya mwamini. Nimeyataja mambo machache dalili za kumkataa Mwana wa Mungu, lakini yako mengi mno yafaa uyaangalie na kuyadhibiti mapema ili yasije yakakutenga na Kristu mkate mtamu wa mbinguni aliyekufanya shamba la mzabibu kwa Damu yake.

Mtume Paulo anakukumbusha kukazia zaidi mambo ya sala na kuyaacha yale yanayokuchelewesha kuunganika na Bwana. Anakuomba uweni mtu wa shukrani daima mbele ya Mungu maana kila ulichonacho ni mali ya Bwana. Kama mmoja atayashika haya amani ya Mungu ipitayo akili zote itakaa ndani mwake daima. Tumsifu Yesu Kristu. Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya Cpps








All the contents on this site are copyrighted ©.