Baba Mtakatifu Francisko, Jumatano akitoa Katekesi kwa mahujaji na wageni alisema,
Mama Kanisa anatufundisha kwamba, matendo ya huruma ni muhimu kwa ajili ya wokovu
wetu. Lakini haitoshi kufanya mema kwa wale walio wema kwetu, kichotakiwa ni kwenda
zaidi ya hao , kuwa wema hasa kwa wale wanaotuchukia. Hii ndiyo silaha ya kuleta
mabadiliko duniani na katika kuwa na dunia iliyo bora zaidi. Ni lazima kufanya mema
kwa wale ambao hawezi kuulipa wema wetu, kama vile Baba wa Mbinguni anavyotenda kwetu,
kutupatia Mwanae Yesu Kristo anayetukomboa dhidi ya minyororo ya dhambi ".
Akizungumza
mbele ya maelfu ya mahujaji waliokuwa wamekusanyika katika uwanja wa Kanisa Kuu la
Mtakatifu Petro Vatican, Papa alisema, Kanisa halifundishi huruma yake kwa mihadhara
kinadharia, lakini kwa njia ya matendo ya watu wa Mungu ambao wanatembea kila mahali,vijijini,
gerezani, mashuleni, na pia wale ambao hufundisha watoto wao kwa kugawana na wengine
kile walicho nacho na kugawana na wale wenye haja, kama ilivyokuwa kwa Matakatifu
Teresa wa Calcutta, aliutoa mkono wake kwa watu wahitaji waliotelekezwa , watu watupu
waliokuwa katika hali ya kufa peke yao mitaani. Hii ndiyo jinsi Mama Kanisa anavyo
fundisha watoto wake kutenda kwa huruma. Kanisa limejifunza njia hii kutoka kwa Yesu
mweyewe, yeye alifundisha kwamba, hii ni muhimu kwa ajili ya wokovu wetu.
Katekesi
ya Papa ilendelea kutafakari juu ya Mama Kanisa, mada iliyoongoza tafakari kadhaa
za nyuma, juu ya Kanisa kama Mama ambaye kupitia imani hulisha waamini wake, kuwaongoza
katika njia ya wokovu, na kuwalinda dhidi ya maovu. Na hivyo katika Katekesi ya
leo, Papa ametoa mafundisho juu ya matendo ya huruma.
Anasema, Kanisa
ni Mwalimu mzuri, ambaye daima hapotezi mwelekeo wa lengo la uwepo wake. Huelekeza
kila muumini wake, anachotakiwa kukifanya, wanafunzi wake na watoto waweza kupata
maana na furaha katika maisha, ambayo ni Ukweli. Katika ukweli wa Injili, jambo
muhimu linalotolewa ni huruma ya Mungu, ya kumtuma Mwana wake , Mungu aliyekuja kukaa
kati yetu ili tuweze kuokolewa. Yesu anasema wazi wazi, wakati wa kukamilisha mafundisho
yake kwa wanafunzi wake:. "Muwe na huruma kama Baba yenu alivyo na huruma" (Lk 6:36)
Na hivyo huu ni wito kwa wakristo wote kwamba Mkristo asiyekuwa na huruma huyo si
Mkristo, kwa kuwa sharti la kuwa Mkristo ni lazima kuwa na huruma, kwa sababu huruma
ni moyo wa Injili na kweli ya mafundisho hayo, kanisa hurudia jambo moja tu nalo
"Muwe na huruma," kama Baba ni, na kama Yesu alivyo na huruma.