2014-09-08 16:03:20

Masista watatu wauawa Burundi


Baba Mtakatifu Francisko, amepeleka salaam zake za rambirambi kwa familia za Masista watatu wanashirika la Mtakatifu Xavery, waliouawa katika nyumba yao ya Kamenge, Kaskazini mwa mji wa Bujumbura siku ya Jumapili. Majina ya Marehemu Masista ni Sista Olga Raschietti, Sista Luchia Pulici na Sr Bernadetta Boggian. Wote wanatajwa kuwa raia wa Italia.

Rambirambi za Papa zimetumwa kwa Mjumbe wake wa Kitume nchini Burundi, Askofu Mkuu Evariste Ngoyagoye na nyingine kwa Mama Mkuu wa Shirika la Masista wa Mtakatifu Xavery, akionyesha kusikitishwa sana na kilichotokea kwa Masista hao. Papa anatumaini damu hii ya watu wa Mungu iliyomwangika bure, itaweza kuwa mbegu ya matumaini katika ujenzi wa udugu wa kweli kati ya jamii ya watu wa Burundi. Na ameahidi kuwakumbuka katika sala zake mashahidi hawa wa Injili , na ukaribu wake kwa shirika, na jumuiya ya waamini nchini Burundi.

Mkuu wa Shirika la Watawa Xaverian nchini Burundi, Padre Mario Pulcini, akithibitisha uwepo wa tukio, ameonyesha hisia kwamba ni tukio la wizi. Na kwamba, Sista Lucia na Sista Olga, waliuawa Jumapili mchana wakati Sista Bernadetta, alikwenda kupokea Masista wengine waliowasili katika uwanja wa ndege tokea Italia.

Wakati aliporejea nyumbani alikutana na hali ya ukimya uliompa wasiwasi na baadaye akiwa na Padre Mario waliona wenzao tayari walikuwa wameuawa ndani ya nyumba yao. Na Sista Bernadetta ameuawa usiku wa kuamkia Jumatatu akiwa katika chumba chake.

Askofu Henry, Jimbo la Parma Italia, kwa niaba ya Kanisa lote la Parma, amepeleka pia niaba ya waamini wa Parma , salaam zake za rambirambi kwa Usharika wa Missionari Xaverians, wakiwafariji kwa sala ya imani kwa Bwana wa Maisha. Askofu pia ametoa ombi kwa Wakristo wa Jimbo la Parma na kwa wote wenye mapenzi mema, kuwakumbuka Masista hawa katika sala zao.







All the contents on this site are copyrighted ©.