2014-08-23 09:36:27

Shule za Kanisa ni vyombo makini vya Uinjilishaji!


Baba Mtakatifu Francisko wakati wa maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa mwaka 2013 mjini Rio de Janeiro, Brazil aliwakumbusha vijana kwamba wao ni sehemu muhimu sana ya utume na maisha ya Kanisa, changamoto ya kushiriki kikamilifu katika maisha ya Kanisa kama wadau wakuu na wala si kama watazamaji. RealAudioMP3

Huu ni mwaliko kwa vijana kusimama kidete kulinda, kujenga na kutetea misingi ya haki, amani, upendo, udugu na mshikamano kati ya watu.

Hili ni jukumu lao na wala hawapaswi kuwasukumia wengine kulitekeleza. Vijana wanapaswa kuwa ni sehemu ya mabadiliko yanayotafutwa na Jamii sehemu mbali mbali za dunia. Baba Mtakatifu aliwaambia vijana kwamba, wao ni chombo makini cha Uinjilishaji Mpya miongoni mwa vijana wenzao.

Papa bado anaendelea kuwaalika vijana kuhakikisha kwamba, wanajitosa kimasomaso kwa ajili ya kutangaza Injili ya Furaha hadi miisho ya dunia, kwa njia ya ushuhuda makini wa maisha yao adili na manyofu, hata kwa wale ambao bado hawaguswi na Habari Njema ya Wokovu.

Kuna uhusiano mkubwa kati ya shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki pamoja na dhamana ya Uinjilishaji Mpya inayovaliwa njuga na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Ili kutambua umuhimu huu, kuna haja kwanza kwa walimu, walezi na wanafunzi wenyewe kufahamu changamoto inayoletwa kwao na Baba Mtakatifu Francisko.

Shule na taasisi za elimu ya juu pamoja na vyuo vikuu vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki, vimekuwa ni vituo vya majiundo makini ya vijana: kiakili, kimaadili, kiroho na kiutu, kwa kuzingatia ubora na viwango vya kitaifa na kimataifa.

Shule, taasisi na vyuo vikuu hivi vimekuwa ni vituo vya majadiliano ya kidini na kiekumene; mahali pa kurithisha imani, maadili na utu wema. Kutokana na dhamana hii, Baba Mtakatifu Francisko anawataka vijana kuwa kweli ni wadau wa Uinjilishaji Mpya kwa njia ya ushuhuda wa maisha na matendo yao adili. Jambo msingi kwa walimu, wazazi na walezi kutambua dhamana na utume wa shule za Kikatoliki katika mchakato wa Uinjilishaji, ili waweze kushiriki kuwajengea watoto na vijana msingi wa imani, maadili na utu wema.

Hapa ni mahali pa kujenga na kuimarisha upendo kwa Mungu na jirani, ili wanafunzi wanaohitimu kutoka katika shule za Kikristo waweze kuwa kweli ni wadau katika kuyatakatifuza malimwengu. Dunia inawahitaji vijana watakaotoka kifua mbele kuwatangazia watu Injili ya Furaha, kwa kutambua kwamba, shule na taasisi hizi ni vyombo makini vya Uinjilishaji Mpya kama ambavyo aliwahi kusema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI alipokuwa anazungumza na Maaskofu kutoka Marekani wakati wa hija yao ya kitume mjini Vatican kunako Mwaka 2012.

Hii ni changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Askofu mwandamizi Eamon Martin wa Jimbo kuu la Armagh nchini Ireland. Anasema, kuna mabadiliko makubwa yanayoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia; mambo ambayo yanaathari zake hata katika sekta ya elimu. Ukanimungu, ubinafsi, mmong’onyoko wa maadili na utu wema, uhuru usiokuwa na mipaka ni kati ya mambo yanayoendelea “kupigiwa debe”, lakini matokeo yake ni vijana wengi wa kizazi kipya kujikatia tamaa na kupoteza mwelekeo wa maisha. Idadi ya vifo vya vijana wanaojinyonga imeongezeka maradufu kwa miaka ya hivi karibuni.

Kuna watu wanaojihesabu kuwa ni Wakristo, lakini kwa miaka mingi wamesahau wapi ambako unapatikana mlango wa Kanisa. Kashfa mbali mbali zilizolikumba Kanisa kwa miaka ya hivi karibuni zinaweza kuwa zimechangia kwa sehemu kubwa. Kumbe, kuna haja sasa kwa wadau mbali mbali wa sekta ya elimu kuanzia kwa wazazi na walezi kuhakikisha kwamba, wanawajengea vijana wa kizazi kipya mazingira yatakayowasaidia kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kutambua kwamba, wazazi ni walimu wa kwanza wa imani kwa watoto wao. Familia ziwe ni shule ya: haki, amani, upendo, mshikamano wa kidugu na utakatifu wa maisha.

Licha ya mwingiliano mkubwa wa wanafunzi kutoka katika dini na madhehebu mbali mbali ya Kikristo, lakini wanafunzi wanapaswa kupewa elimu ya dini au maisha ya kiroho kwani hii ni haki yao msingi. Elimu inayotolewa na Mama Kanisa anasema Askofu mwandamizi Eamon Martin inamlenga mtu mzima: kiroho na kimwili na kwamba, Yesu Kristo anatoa maana halisi ya maisha na historia ya binadamu. Shule, taasisi za elimu na vyuo vikuu vya Kikatoliki havina budi kuendeleza utamaduni na Mapokeo ya Kanisa kuhusu elimu.

Baba Mtakatifu Francisko anawakumbusha Wakristo kwamba, haitoshi kuwa na jina la Kikristo, bali kutambua kwamba, katika hija ya maisha wamebahatika kukutana na Yesu ambaye ni dira na kiongozi wao mkuu katika hija ya maisha yao hapa duniani.

Changamoto kubwa kwa sasa ni kuhakikisha kwamba, waamini wanawatangazia jirani zao Injili ya Furaha kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji, inayomwilishwa katika matendo adili. Wainjilishaji wawe ni watu wenye furaha inayobubujika kutoka katika undani wa maisha yao kwa vile wamekutana na Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.

Ni mwaliko wa kuwaonjesha wengine upendo na huruma ya Mungu inayobubujika katika Neno la Mungu na Maisha ya Kisakramenti. Kwa hakika Wakristo wanapaswa kuwa kweli ni chumvi na mwanga wa dunia. Wanahamasishwa kuyatakatifuza malimwengu. Wawe ni mashahidi wa Imani wanayokiri, adhimisha, mwilisha na kusali, kama ambavyo inafafanuliwa kwenye Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki.

Wanafunzi wajengewe utamaduni wa kupenda kusoma na kulitafakari Neno la Mungu ili waweze kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai. Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, yawasukume waamini kuwa kweli ni Wamissionari wa huruma na upendo wa Mungu kati ya watu wake. Vijana wafundwe kupenda Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu, kwani hii ndiyo “injini” ya maisha na utume wa Kanisa. Fumbo la Ekaristi Takatifu liwe ni kiini cha mshikamano wa upendo na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Watu waguswe na mahangaiko ya jirani zao, tayari kuwaonjesha ukarimu unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Vyama vya kitume katika shule na taasisi za elimu vinaweza kuwa ni msaada mkubwa katika ujenzi wa mshikamano na maskini. Kanisa katika sekta ya elimu, kamwe lisiwasahau watoto wa maskini, ambao wanaweza kubadili na kuboresha maisha yao kwa njia ya elimu makini.

Askofu mwandamizi Eamon Martin anasema, kuna haja ya kujenga na kuimarisha uhusiano kati ya: Familia, Shule na Parokia, kwani makundi haya matatu yanaunda kwa kiasi kikubwa Jopo la Wadau wa Uinjilishaji Mpya. Watoto na vijana wafundishwe na kurithishwa imani, maadili na utu wema. Waendelezwe kiakili kwa njia ya elimu makini na kufundwa barabara katika Katekesi.

Mambo yote haya yataliwezesha Kanisa kuwajengea watoto na vijana uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa. Vijana wanaweza kushirikisha vipaji na karama zao, furaha na matumaini yao kwa leo na kesho iliyo bora zaidi. Shule za Kikatoliki ni chanda na pete katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya.

Taarifa hii imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.