Jielekezeni zaidi katika kujibu wito wenu wa maisha ya kitawa!
Shirikisho la Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume nchini Canada mwaka 2014
linafanya kumbu kumbu ya miaka 60 tangu lilipoanzishwa, changamoto kubwa iliyoko mbele
ya watawa kwa wakati huu ni kuhakikisha kwamba, Jumuiya za kitawa zinajielekeza zaidi
katika kujibu wito wao wa kukutana na Mwenyezi Mungu, tayari kujisadaka kwa ajili
ya Kristo na Kanisa lake kwa njia ya ushuhuda wa huduma makini zinazotolewa na watawa
katika Kanisa na Jamii kwa ujumla.
Shirikisho
hili linaadhimisha kumbu kumbu hii, wakati Mama Kanisa anajiandaa kuadhimisha Mwaka
wa Watawa Duniani utakazozinduliwa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili ya kwanza
ya Kipindi cha Majilio kwa Mwaka 2014. Katika ujumbe wake kwa wakuu wa Mashirika,
Askofu mkuu Paul –Andrè Durocher, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Canada, CCCB
anawahimiza watawa kuwa ni vyombo makini vya Uinjilishaji Mpya kwa kujikita katika
wongofu wa shughuli za kichungaji pamoja na kujiandaa kikamilifu kwa ajili ya maadhimisho
ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia itakayoadhimishwa mjini Vatican
kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba 2014.
Katika mchakato wa Uinjilishaji
Mpya mambo makuu yafutayo yanapewa kipaumbele cha kwanza kwa Familia ya Mungu nchini
Canada. Jambo la kwanza ni ushuhuda unaojikita katika maisha ya kijumuiya kama watu
waliokutana na Yesu katika hija ya maisha yao, wakaacha yote na kuamua kumfuasa kama
ilivyokuwa kwa Wakristo wa Kanisa la mwanzo. Hii ni Jumuiya ya Waamini inayojisadaka
kwa ajili ya huduma kwa Mungu na jirani.
Mashirika ya kitawa na kazi za kitume
yanapaswa kumwilisha karama za Mashirika yao kama kielelezo makini cha ushuhuda wao
kwa Kanisa mahalia. Jumuiya za Kitawa ziwe ni kielelezo cha huduma inayofanywa kwa
Jamii kwa kuondokana kabisa na chachu ya ubinafsi unaoweza hata kujionesha kwa njia
ya Mashirika ya kitawa na Kazi za kitume.
Mashirika yote yanahamasishwa kushirikiana
kwa pamoja kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa mahalia, kwa kuwasaidia watu kumwendelea
Mwenyezi Mungu kwa njia ya Kanisa, ili kushiriki katika mchakato wa ujenzi wa Ufalme
wa Mungu unaosimikwa katika msingi wa haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati.
Mashirika ya kitawa yawe ni chachu ya hija ya upatanisho, matumaini, uponyaji na upyaisho
wa maisha ya watu.
Baba Mtakatifu Francisko ana matumaini makubwa kwa watawa
kwamba, watachangia kwa kiasi kikubwa katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya dhamana
ya Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Watawa washiriki katika
maisha na utume wa familia kwa kuwasaidia wanandoa na familia katika maisha ya kiroho
na kimwili kwa njia ya sala, mafungo, kazi na mashauri mbali mbali. Watawa wajitambue
kwamba, hata wao ni sehemu na matunda ya familia ya Kikristo, wanaopaswa kushuhudia
tunu msingi za maisha ya kifamilia kwa njia ya maisha ya kijumuiya ndani ya mashirika
yao, kwa njia ya huduma inayoonesha ile furaha ya ndani kwa kuongozwa na moyo, ari
na upendo kwa njia ya huduma.
Watawa wanapaswa kushirikiana na Maaskofu mahalia
kama inavyobainishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika ile hati
ya Upendo Mkamilifu. Watawa washiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa,
pamoja na kuendelea kulisaidia Kanisa kuonesha ule umuhimu wa kuwa kweli ni Familia
ya Mungu inayowajibika. Watawa waoneshe kwamba, wao ni Jumuiya ya waamini, inayojikita
katika imani, upendo wa kidugu, huruma na unyenyekevu. Imehaririwa Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.