Waelimisheni watu juu ya utunzaji bora wa mazingira!
Baraza la Maaskofu Katoliki Italia katika maadhimisho ya Siku ya utunzaji bora wa
mazingira kitaifa inayoadhimishwa hapo tarehe 1 Septemba 2014 kwa kuongozwa na kauli
mbiu “Elimisha juu ya utunzaji bora wa mazingira, kwa ajili ya ustawi wa nchi na miji
yetu”.
Uchafuzi wa
mazingira ni hali ambayo inaendelea kuhatarisha maisha ya viumbe hai ndani na nje
ya Italia, kiasi hata cha kuharibu agano kati ya Mwenyezi Mungu na viumbe wake. Watu
wamegeuka kuwa ni waharibifu wakubwa wa mazingira, kiasi kwamba, damu ya watu wasiokuwa
na hatia inaendelea kumwagika siku hadi siku; watu wameshikwa na hofu kutokana na
matumizi ya nguvu.
Licha ya mambo yote haya, lakini Mwenyezi Mungu ameendelea
kuwa mwaminifu kwa agano lake, kama yanavyoonesha Maandiko Matakatifu, ili kusaidia
mchakato wa ujenzi wa udugu sanjari na kutunza uzuri wa kazi ya uumbaji na vyote vilivyomo.
Tangu mwanzo Mwenyezi Mungu aliumba bustani nzuri akampatia mwanadamu kuitunza na
kuiendeleza. Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa kichungaji, Injili ya
Furaha anasema kwamba, mwanadamu amepewa dhamana ya kulinda na kutunza mazingira kwa
ajili ya viumbe wengine pia.
Uharibifu wa mazingira ni kosa ambalo linafanywa
na binadamu, kumbe kuna haja ya kujutia kosa hili, kwa kuhakikisha kwamba, mwanadamu
anajitahidi kutunza mazingira ili kwamba, pale anapopitia pasibaki kuwa ni nyayo za
uharibifu na kifo, mambo yatakayoathiri hata kizazi kijacho.
Bustani ambayo
imeharibiwa ni kielelezo cha kumong’onyoka kwa maadili na utu wema, mambo yanayojionesha
ndani na nje ya maisha ya mwanadamu. Tatizo kubwa linalomwandama mwanadamu katika
ulimwengu mamboleo ni uchafuzi mkubwa wa mazingira unaosababishwa na uchu wa mali
na faida kubwa, hali inayosababisha watu kuwa na matumizi mabaya ya mazingira, kiasi
kwamba, uchafuzi huu umekuwa ni chanzo cha magonjwa kama vile Saratani. Watu hawasutwi
na dhamiri nyofu na wanaona kana kwamba, yote ni sawa tu! Lakini kuna haja kwa watu
kubadilisha mtindo na mfumo wa maisha.
Mafuriko na matetemeko ya ardhi yamekuwa
ni chanzo kikuu cha vifo na uharibifu mkubwa wa makazi ya watu na miundo mbinu, kiasi
kwamba, waathirika wanapofikwa na majanga haya, kunakuwepo na mshikamano wa hisia
bila hata kugusa undani wa mtu. Watu wanafahamu vyanzo vya majanga haya lakini bado
wanaonesha mioyo migumu, hawataki kubadilika.
Hapa kuna haja ya kujenga na
kudumisha utamaduni wa kuzuia majanga, kuliko mtindo wa sasa kuanza kushughulikia
majanga baada ya kuona athari zake. Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa
Injili ya Furaha anawaalika watu kutaabikiana na kusaidiana kwa hali na mali, kama
kielelezo cha upendo na mshikamano wa kidugu.
Changamato kubwa kwa sasa ni
kuelimisha dhamiri nyofu kwa kila mtu kwani utunzaji bora wa mazingira ni dhamana
ya wote. Kazi ya kurithisha dhamana hii ifanywe kuanzia shuleni kwani mazingira bora
ni chanzo cha matumaini hata katika sekta nyingine kama vile: kilimo, utalii na maendeleo
endelevu. Sera na mikakati ya uchumi isaidie kuwa na matumizi bora ya ardhi, kwa kutengeneza
fursa za ajira pasi na kuharibu mazingira. Katekesi makini isaidie juhudi hizi miongoni
mwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema.
Umefika wakati wa vyombo vinavyohusika
na utunzaji bora wa mazingira kuwashughulikia watu wanaoharibu mazingira kisheria.
Wananchi wawajibike kulinda na kutunza mazingira kwani ni kwa ajili ya ustawi na maendeleo
yao. Wale wanaochafua mazingira walipe fidia kutokana na uharibifu huu. Lakini yote
haya yanaweza kufanikiswa ikiwa kama kutakuwepo na mshikamano wa dhati kati ya watu
ndani ya Jamii.
Kila mtu ajisikie kuwa ni sehemu ya utunzaji bora wa mazingira
na wala si mtazamaji kama inavyojionesha kwa watu wengi wa nyakati hizi. Watu wawe
na ujasiri wa kubadili mfumo na mitindo ya maisha, kwa kuwa na matumizi ya kiasi,
ili kupunguza uchafuzi na uharibifu wa mazingira. Ikumbukwe kwamba, mazingira bora
ni chanzo kikuu cha fursa za ajira kwa vijana. Vijana wasimame kidete kulinda na kutetea
mazingira.
Imehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.