2014-08-21 13:33:54

Utajiri wa mafuta kutoka Uwanda wa Delta Nigeria unaweza kuwa ni chanzo cha majanga ya kitaifa!


Askofu Lucius Ugorji wa Jimbo katoliki Umuahia, nchini Nigeria anasema kwamba, utajiri mkubwa wa mafuta ulioko kwenye Uwanda wa Delta, Nchini Nigeria unaweza kuwa ni chanzo cha majanga na uvunjifu wa misingi ya haki, amani na utulivu nchini Nigeria, ikiwa kama haki na utawala wa sheria havitazingatiwa. Askofu Ugorji ameyasema hayo hivi karibuni alipokuwa anazungumza katika semina ya siku moja ya wawekezaji wakuu katika Uwanda wa Delta.

Askofu Ugorji amepembua kwa kina na mapana mambo mbali mbali yanayoashiria ukosefu wa uongozi bora na utawala wa sheria katika eneo hili ambalo lina utajiri mkubwa wa mafuta ambayo yamekuwa pia ni chanzo cha kinzani na migogoro ya kijamii.

Kuna kiasi kikubwa cha fedha inayozalishwa katika eneo hili, lakini fedha hii inatakatishwa na wajanja wachache na kuingizwa tena kwenye mfumo wa biashara. Kuna baadhi ya watu binafsi na makundi ya watu yanayotaka kubinafisha uzalishaji wa mafuta ghafi kutoka Uwanda wa Delta, madhara yake yanaweza kuwa ni makubwa kwa wananchi wa Nigeria kwani hiki kinaweza kuwa ni chanzo cha uvunjifu wa amani na utulivu nchini Nigeria.

Askofu Lucius Ugorji anahoji, Je, inawezekana vipi kudhibiti uzalishaji wa mafuta ghafi, ili usiwe ni chanzo cha majanga nchini Nigeria? Je, haiwezekani kabisa kwamba, fedha inayozalishwa katika ukanda huu ikatumika kwa ajili ya kugharimia kampeni za chaguzi mbali mbali nchini Nigeria na matokeo yake, watu hawa wakiishakuingia madarakani wanalazimika kutekeleza matakwa ya wafadhili wao wakati wa Kampeni za uchaguzi.

Bado kuna ufisadi na wizi mkubwa wa mali ya umma kwenye Uwanda wa Delta mambo ambayo yanapaswa kudhibitiwa na Serikali kwa kuzingatia utawala wa sheria na kanuni maadili, daima mafao ya wengi yakipewa kipaumbele cha kwanza. Kuna uchafuzi mkubwa wa mazingira katika eneo hili kutokana na kuvuja kwa mafuta katika mkondo wa maji, mambo yanayofanywa wakati mwingine kwa njia ya hujuma. Mambo yote haya ni tishio kubwa katika utunzaji bora wa mazingira.







All the contents on this site are copyrighted ©.