2014-08-21 11:54:59

Jimbo Katoliki Kitui, Kenya linasherehekea Jubilee ya Miaka 50 tangu kuanzishwa kwake!


Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, Jumamosi tarehe 16 Agosti 2014 ameiongoza Familia ya Mungu, Jimbo Katoliki la Kitui, Kenya kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa kuadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu Jimbo hili lilipoanzishwa na Mapadre wa Roho Mtakatifu. Kardinali Njue amewataka waamini Jimboni humo kujifunga kibwebwe ili kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji ulioanzishwa na Wamissionari Jimboni humo!

Kardinali Njue amewaambia waamini kwamba, Wamissionari walipandikiza mbegu ya Ukristo, wakiwa na nia ya kutaka kuhakikisha kwamba, Habari Njema ya Wokovu inawafikia pia wananchi wa Kitui. Maadhimisho haya ni fursa makini ya kufanya upembuzi yakinifu ili kuangalia ikiwa kama kweli ile mbegu ya Ukristo iliyopandwa na Wamissionari imekuwa na kuzaa matunda ya toba, wongofu na utakatifu wa maisha.

Ibada hii imehudhuriwa na idadi kubwa ya Maaskofu kutoka Kenya pamoja na kupata baraka ya uwepo wa Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya. Rais Kenyatta amelipongeza Kanisa Katoliki kwa kazi kubwa ambalo limewafanyia wananchi wa Kenya katika kipindi cha miaka 50 iliyopita. Waamini wamepata chakula cha maisha ya kiroho, lakini pia Kanisa limeisaidia Serikali kutekeleza barabara wajibu na dhamana yake kwa wananchi wa Kenya, hususan katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Kanisa nchini Kenya limechanfia kwa kiasi kikubwa katika maboresho ya maisha ya wananchi wa Kenya, changamoto kwa Serikali na Kanisa kuendelea kushirikiana katika utekelezaji wa mikakati ya maendeleo kwa wananchi wa Kenya.

Katika tukio hili, Askofu Anthony Muheria wa Jimbo la Kitui, ameadhimisha Kumbu kumbu ya miaka 10 tangu alipowekwa wakfu kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Embu, ambako aliwahudumia watu wa Mungu kwa miaka minne na baadaye akateuliwa kuongoza Jimbo Katoliki la Kitui na tayari miaka sita imekwisha yoyoma. Jimbo Katoliki la Kitui lilimegwa kutoka Jimbo kuu la Nairobi kunako mwaka 1956 na Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI na kunako mwaka 1963 Monsinyo William Dunne, akateuliwa kuwa Askofu wa kwanza wa Jimbo Katoliki la Kitui. Jimbo hili limewahi kuhudumiwa na Marehemu Askofu mkuu Bonoface Lele kabla ya kukabidhiwa kwa Askofu Muheria.

Jimbo Katoliki la Kitui linatoa huduma za kichungaji katika elimu, afya na maendeleo endelevu, huduma inayosimamiwa na Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki Kenya, Caritas Kenya.







All the contents on this site are copyrighted ©.