2014-08-20 08:42:35

Mchakato wa majadiliano kati ya Kanisa na walimwengu!


Kanisa linalojikita katika majadiliano ya kina: Mapitio ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, ndiyo kauli mbiu itakayoongoza Kongamano la kitaifa la siku mbili litakalofanyika nchini Ubelgiji kuanzia tarehe 26 hadi tarehe 28 Oktoba 2014. Kati ya washiriki wakuu wa Kongamano hili ni pamoja na Kardinali Gerhard Muller, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa. RealAudioMP3

Itakumbukwa kwamba, maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican yalifanyika kuanzia mwaka 1962 hadi mwaka 1965 na hapa ukawa ni mwanzo wa Kanisa linalojadili mintarafu Ufunuo wa Mungu, kwa kutoa kipaumbele cha pekee majadiliano ya kidini na kiekumene na waamini wa dini mbali mbali pamoja na tamaduni zilizoko katika ulimwengu mamboleo.

Baraza la Maaskofu Katoliki Ubelgiji linasema kwamba, majadiliano ya kidini na kiekumene yanafumbatwa katika misingi ya ukweli, uwazi, upendo na mshikamano wa dhati. Ni mchakato wa kuheshimiana na kuthaminiana kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Kwa mwelekeo huu, Familia ya Mungu nchini Ubelgiji itajadili kuhusu: nyaraka za Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kuhusiana na: majadiliano ya kidini na kiekumene; Utangazaji wa Habari Njema kwa Watu wa Mataifa, Kanisa katika Ulimwengu pamoja na kuangalia changamoto zinazoendelea kujitokeza katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, zinazohitaji mikakati ya Uinjilishaji Mpya kama anavyofafanua kwa kina Baba Mtakatifu Francisko.

Maadhimisho ya Kongamano hili yatafanyika kwa kipindi cha siku tatu, katika maeneo matatu tofauti, ili kuwawezesha waamini kushiriki kikamilifu katika tukio hili la kihistoria. Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya ufunguzi, itaadhimishwa kwenye Kanisa kuu la Koelberg mjini Brussels na Askofu mkuu Andrè-Joseph Leonard. Wajumbe wa kongamano hili pamoja na mambo mengine watapembua kwa kina na mapana tema kuhusu “Utamadunisho na Ugunduzi” mahusiano yaliyopo kati ya Mapokeo ya Kikristo na utamaduni mamboleo.








All the contents on this site are copyrighted ©.