2014-08-19 10:20:19

Sitisheni mateso ya watu wasiokuwa na hatia!


Askofu mkuu Dieudonnè Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui, Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, katika mahubiri yake wakati wa maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu hivi karibuni, amewataka viongozi wa Serikali na wanasiasa kuhakikisha kwamba, wanafanya maamuzi magumu ili kuokoa maisha ya watu na mali zao Nchini Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati.

Askofu mkuu Nzapalainga kwa niaba ya wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi maalum nchini humo, amemwomba Waziri mkuu mpya Mahamat Kamoun, kufanya maamuzi magumu, ili kuokoa maisha ya watu wanaoendelea kuteseka kutokana na machafuko ya kisiasa nchini humo. Bado watu wanauwawa kikatili licha ya Kikundi cha Seleka na Wanajeshi wa Balaka kutiliana sahihi mkataba wa kusitisha mapigano hapo tarehe 23 Julai 2014 mjini Brazzaville.

Tarehe 14 Agosti 2014 Waziri mkuu Mahamat Kamoun, aliyeteuliwa hivi karibuni na Rais Samba Panza aliapishwa rasmi na kuanza kutekeleza majukumu yake kama Waziri mkuu wa Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati.







All the contents on this site are copyrighted ©.