2014-08-19 10:44:46

Baba Mtakatifu Francisko amewasha moto nchini Korea!


Askofu Peter Kang U-il, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Korea ya Kusini anasema, hija ya Baba Mtakatifu nchini mwao imekuwa na mafanikio makubwa katika maisha ya watu kiimani na imeacha chapa na alama ya kudumu kwa maisha ya waamini na wananchi wa Korea katika ujumla wao. Hili ni tukio ambalo limefuatiliwa kwa umakini mkubwa na vyombo vya habari ndani na nje ya Korea.

Askofu Peter anasema, kwake, kilele cha hija ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Korea kilikuwa pale alipowatembelea watoto wenye mtindio wa ubongo, akawakumbatia, akawafriji na kuwabariki. Hawa ni watoto wanaoishi katika mazingira magumu na hatarishi, ni watoto walitelekezwa na wazazi wao kutokana na ulemavu, ni watoto waliokuwa wanachungulia kaburi, lakini wameonja upendo mkuu kutoka kwa Mama Kanisa.

Baba Mtakatifu alitumia muda mrefu kumsalimia kila mtoto, tukio lililopelekea kusitishwa kwa Sala ya Masifu ya Jioni kati ya Baba Mtakatifu na Watawa. Lakini Baba Mtakatifu mwenyewe aliwaambia kwamba, Sala ni muhimu sana katika maisha ya waamini, lakini huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ina umuhimu wa pekee mbele ya Mwenyezi Mungu, kwani hii ni sala inayomwilishwa katika matendo!

Baba Mtakatifu alipenda kukazia umuhimu wa Kanisa kushikamana na maskini, ili kuwaonjesha huruma na upendo wa Mungu. Huu ndio ujumbe muhimu sana kwa waamini na wananchi wa Korea katika ujumla wao, Kanisa halina budi kujitambulisha na kuwahudumia maskini!

Askofu Peter anasema, Baba Mtakatifu amewaachia wananchi wa Korea shauku kubwa katika maisha yao kutokana na unyenyekevu pamoja na kuguswa na maisha ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Tukio la kuwatangaza Mashahidi na wafiadini wa Korea kuwa ni Wenyeheri. Hii ni changamoto kubwa kwa waamini nchini Korea kuendelea kuonesha imani yao kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya ushuhuda wa maisha na imani inayomwilishwa katika matendo.

Faraja iliyotolewa na Baba Mtakatifu kwa watu walioguswa na ajali ya kuzama kwa Meli Sewol, imewapatia wananchi wengi faraja baada ya kuondokewa na wapendwa wao. Baba Mtakatifu aliweza kuzungumza na kuwapatia neno la faraja, kama mbegu ya kuponya madonda ya ndani, tayari kuanza tena safari ya maisha, wakiwa na mwelekeo mpya.

Hapa Baba Mtakatifu aliguswa na mahangaiko yao, akayashiriki kwa imani na matumaini. Hiki kilikuwa ni kielelezo cha uwepo wa karibu katika hija yao ya maisha, inayohitaji kweli uponyaji wa ndani. Watu hawa hawatasahau tukio hili katika maisha yao.

Ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa vijana Barani Asia ni changamoto endelevu inayowataka vijana kusimama imara katika misingi ya imani, maadili na utu wema. Amani na Upatanisho, Umoja wa Kitaifa na Udugu ni mambo msingi ambayo wananchi wote wa Korea wanapaswa kuyafanyia kazi, ili kuimarisha upendo na mshikamano wa kitaifa, wakiwa wanatembea kwa pamoja kama ndugu wamoja!







All the contents on this site are copyrighted ©.