2014-08-18 14:14:23

Sala kuhusu changamoto za kifamilia!


Mama Kanisa anatarajia kuadhimisha Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayofanyika mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba, 2014. Mababa wa Sinodi wataangalia kwa kina na mapana: fursa, changamoto na matatizo yanayozikablia familia, ili kuwatangazia watu wa mataifa Injili ya Familia ya Kikristo.

Ifuatayo ni sala inayogusa baadhi ya matatizo na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika familia: Ebu angalia na linganisha na maisha ya familia yako, ili uweze kufanya maboresho makubwa zaidi katika maisha na utume wa familia.

Ee Mungu wa Upendo na Amani, tunakuomba utufanye sisi tuwe vyombo vya Amani yako katika Familia zetu kwa njia ya Sala hii ya Familia Kupendana, kusameheana na kutaabikiana. Na sasa tusali.
Penye Familia yenye CHUKI, tupeleke UPENDO,
Penye Familia yenye MAFARAKANO, tupeleke MAELEWANO
Penye Familia yenye MAHANGAIKO, tupeleke UTULIVU
Penye Familia yenye MATESO, tupeleke FARAJA
Penye Familia yenye MASHAKA, tupeleke UHAKIKA
Penye Familia yenye UWONGO, tupeleke UKWELI

Penye Familia yenye HUZUNI, tupeleke FURAHA
Penye Familia yenye MAJERAHA, tupeleke UPONYAJI
Penye Familia yenye GIZA, tupeleke MWANGA
Penye Familia yenye UKANDAMIZAJI, tupeleke HURUMA
Penye Familia yenye UJINGA, tupeleke ELIMU,HEKIMA NA BUSARA.

Penye Familia yenye UBINAFSI, tupeleke UKARIMU
Penye Familia yenye RUSHWA, tupeleke HAKI
Penye Familia yenye UBAGUZI, tupeleke USAWA
Penye Familia yenye UKABILA, tupeleke UDUGU
Penye Familia yenye UFISADI, tupeleke UAMINIFU.

Penye Familia yenye DHARAU, tupeleke HESHIMA
Penye Familia yenye MAJIVUNO, tupeleke UNYENYEKEVU,
Penye Familia yenye MAUAJI, tupeleke UHAI
Penye Familia yenye WASIWASI, tupeleke MATUMAINI
Penye Familia yenye UPAGANI, tupeleke INJILI,
Penye Familia yenye VIFUNGO, tupeleke MSAMAHA.

Penye Familia yenye USHIRIKINA, tupeleke UCHAJI
Penye Familia yenye VURUGU, tupeleke AMANI,
Penye Familia yenye UADUI, tepeleke URAFIKI.

Ee Mungu uzifanye familia zetu ziige mfano wa Familia yako Takatifu ya Nazareti, ya Yesu, Maria na Yosefu. Amina!

Bikira Maria Malkia wa Familia, utuombee!
Mtakatifu Yosefu Mlinzi wa Familia zetu, utuombee!
Mtakatifu Yosefu Kitisho cha mashetani, utuombee!
Mtakatifu Yosefu uzuri wa mwenendo wa nyumbani, utuobee!
Moyo wa Yesu chemchemi ya uzima, utakatifu na faraja zote, Utuhurumie!








All the contents on this site are copyrighted ©.