2014-08-18 09:57:00

Misa ya kuombea amani na upatanisho nchini Korea!


Baba Mtakatifu Francisko katika siku yake ya mwisho nchini Korea, Jumatatu tarehe 18 Agosti 2014, ameanza kwa kukutana na kusalimiana na viongozi wa kidini nchini Korea na baadaye ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuombea amani na upatanisho nchini Korea, ibada ambayo imehudhuriwa pia na viongozi wa Serikali kutoka Korea ya Kusini. Ibada hii imeadhimishwa kwenye Kanisa kuu la Meyong-dong la Jimbo kuu la Seoul, Korea.

Baba Mtakatifu ameanza Ibada hii kwa kumwomba Mwenyezi Mungu neema ya amani na upatanisho kwa ajili ya Familia ya Mungu nchini Korea. Liturujia ya Neno la Mungu imejikita katika umoja unaopata chimbuko lake kutoka kwa Mwenyezi Mungu, baada ya watu kutopea katika utengano na mgawanyiko. Mwenyezi Mungu anawapatia ahadi ya kuwaunganisha tena, ikiwa kama wataheshimu na kutii amri zake kutoka katika undani wa mioyo yao!

Baba Mtakatifu anasema upatanisho, umoja na amani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayofumbatwa katika toba na wongofu wa ndani. Hii ni changamoto ya kufanya mabadiliko ya kweli kutoka katika undani wa moyo wa mwanadamu, hali inayoweza kuleta mabadiliko makubwa katika maisha na historia ya mtu binafsi na kama Jamii ya watu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema mang'amuzi haya yanajidhihirisha kwa namna ya pekee katika mazingira ya historia ya wananchi wa Korea; haya ni mang'amuzi ya utengano na kinzani ambazo zimekuwepo kwa takribani miaka sabini. Mwenyezi Mungu anawaalika waamini na wananchi wa Korea katika ujumla wao kutubu na kumwongokea; kufanya tafakari ya kina kuhusu mchango wao katika ubora wa ujenzi wa Jamii inayojikita katika haki na ubinadamu.

Wananchi wa Korea wanaalikwa kutafakari kama mtu binafsi na Jumuiya, jinsi wanavyotolea ushuhuda wa Kiinjili kwa ajili ya maskini, watu wanaotengwa na kusukumizwa pembezoni mwa Jamii; kwa watu wasiokuwa na fursa za ajira au wale ambao wametengwa kutoka kwenye mchakato wa maendeleo ya wengi. Mwenyezi Mungu anawaalika kama Wakristo na kama wananchi wa Korea kuachana na mawazo ya kudhaniana vibaya, kinzani na ushindani usiokuwa na tija wala mashiko.

Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake anasema Yesu anawataka kuamini kwamba, msamaha ni mlango unaowaelekeza watu katika upatanisho. Anawataka wafuasi wake kujikita katika upatanisho bila kubakiza kinyongo. Anawataka kufanya mabadiliko ya kweli na anawajalia neema ya kutekeleza kazi hii. Msalaba wa Kristo unaonesha ile nguvu ya Mwenyezi Mungu katika kutuliza utengano, kuganga madonda na kujenga tena mahusiano yanayojikita katika upendo wa kidugu.

Na kwa mawazo haya, Baba Mtakatifu anahitimisha mahubiri yake nchini Korea, akiwataka waamini nchini Korea kuwa na imani katika nguvu ya Msalaba wa Kristo; kujenga na kuimarisha ari na moyo wa urafiki kati ya Wakristo, waamini wa dini mbali mbali pamoja na watu wenye mapenzi mema nchini humo, watu ambao wana taka kuona mafanikio ya mustakabali wa Korea; kwani wao watakuwa ni chachu ya Ufalme wa Mungu nchini Korea.

Baba Mtakatifu Francisko amewaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema nchini Korea kusali ili kumwomba Mwenyezi Mungu aweze kuwakirimia fursa za majadiliano, mikutano na moyo wa kutaka kuvuka vikwazo vya kutowajali wengine; bali kwa kuendeleza ukarimu kwa kuwasaidia maskini pamoja na kutambua kwa mapana zaidi ukweli kwamba, wananchi wote wa Korea ni ndugu na watu wa familia moja!

Wakati wa Sala ya Waamini, Baba Mtakatifu Francisko amemkumbuka na kumwombea Kardinali Fernando Filoni ambaye alipaswa kuwa kwenye msafara wa Baba Mtakatifu wakati wa hija yake ya kitume nchini Korea, lakini akalazimika kwenda Iraq kumwakilisha, kama kielelezo cha mshikamano wa dhati na watu wanaoteseka na kudhulumiwa nchini Iraq. Baba Mtakatifu anamwomba Yesu Kristo ili aweze kuwa karibu naye katika maisha na utume wake huko Iraq.







All the contents on this site are copyrighted ©.