Vijana simameni kidete kwani mna wajibu na dhamana!
Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili jioni tarehe 17 Agosti 2014, amehitimisha maadhimisho
ya Siku ya Sita ya Vijana Barani Asia iliyokuwa inaongozwa na kauli mbiu "Ondoka,
uangaze, kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa Bwana umekuzukia" kwa Ibada ya
Misa Takatifu iliyoadhimishwa kwenye Uwanja wa Boma la Haemi, lililojengwa kunako
mwaka 1421 kama kinga dhidi ya maharamia na kunako mwaka 1490 boma hili likageuzwa
kuwa ni kituo cha kijeshi.Tukio hili limehudhuriwa na vijana kutoka katika mataifa
ishirini na mbili.
Baba Mtakatifu katika mahubiri yake amekiri kwamba, tema
iliyochaguliwa na Maaskofu katika maadhimisho ya Siku ya Sita ya Vijana Barani Asia
inatoa mwelekeo wa pekee katika maisha na utume wa Kanisa miongoni mwa vijana. Huu
ni ushuhuda mkubwa unaoungama imani kwa Kristo. Vijana Barani Asia, simameni, hii
ni dhamana na wajibu ambao kweli vijana wanapaswa kuutekeleza katika maisha yao.
Baba
Mtakatifu anasema, vijana kutoka sehemu mbali mbali za Bara la Asia wamekusanyika
nchini Korea. Bara la Asia lina utajiri mkubwa wa mapokeo, falsafa na dini na kwamba,
huu ni uwanja ambao waamini wanapaswa kuutumia ili kushuhudia imani yao kwa Kristo
ambaye ni njia, ukweli na uzima.
Vijana wanakumbushwa kwamba, wao ni watoto
wa Bara la Asia, wana haki na dhamana ya kushiriki kikamilifu katika maisha ya jamii
zao. Baba Mtakatifu anawataka vijana kuondokana na woga ili kupeleka hekima ya imani
katika medani mbali mbali za maisha ya kijamii. Vijana waone na kupenda kile ambacho
ni chema, kizuri na kweli kutoka katika tamaduni na mapokeo yao. Watambue kwamba,
Injili ina nguvu ya kuweza kusafisha, kuinua na kukamilisha hazina hii kubwa.
Vijana
wawe makini kung'amua kile ambacho ni kinyume cha imani ya Kanisa Katoliki, yaani
mambo ambayo yanakwenda kinyume cha maisha ya neema iliyomiminwa mioyoni mwao kwa
njia ya Sakramenti ya Ubatizo; wawe waangalifu kwa tamaduni mamboleo zinazoweza kuwatumbukiza
katika dhambi, rushwa na hatimaye, kuwasukumizia katika kifo.
Baba Mtakatifu
Francisko anasema ujana ni kielelezo cha matumaini makubwa, nguvu na utashi mwema,
mambo yanayogubika maisha ya ujana. Vijana wanachangamotishwa na Mama Kanisa kumwachia
nafasi Yesu, ili aweze kuwaletea mabadiliko yanayojikita katika matumaini ya Kikristo
na nguvu zao katika fadhila za kimaadili; matashi yao mema yageuzwe katika upendo
unaothubutu kujisadaka.
Baba Mtakatifu Francisko anawakumbusha vijana kwamba
wao ni matumaini ya Kanisa kwa siku za usoni na sehemu muhimu sana inayopendwa na
Kanisa kwa wakati huu. Anawataka vijana kuendelea kuungana, ili kulijenga Kanisa ambalo
ni takatifu zaidi, Kanisa la Kimissionari na linalojikita katika unyenyekevu; Kanisa
ambalo linampenda na kumwabudu Mwenyezi Mungu; Kanisa linalojielekeza zaidi katika
huduma kwa maskini, wapweke, wagonjwa na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Baba
Mtakatifu anawaambia vijana kutoka Barani Asia, kusimama imara kama kielelezo cha
dhamana ambayo wanakabidhiwa na Yesu mwenyewe. Wanatakiwa kuwa macho na makini, ili
mashikinikizo, majaribu na dhambi zao au zile za jirani zao zisivuruge umakini wao
kuhusu uzuri wa utakatifu wa maisha kwa ajili ya Furaha ya Injili.