2014-08-17 10:24:07

Mama wakuu wa Mashirika ya Kitawa kutoka katika nchi za AMECEA wameanza mkutano wao mjini Lusaka


Shirikisho la Mabaraza ya Watawa wa Kike Afrika Mashariki, ACWECA, Jumapili tarehe 17 Agosti 2014 limefungua mkutano wake wa kumi na sita Jimbo kuu la Lusaka, Zambia kwa kuongozwa na kauli mbiu "Nenda, usiogope, kahudumie". Mkutano huu unawajumuisha Mama wakuu wa Mashirika ya Kitawa 150 kutoka katika Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA.

Ni mkutano unaohudhuriwa pia na viongozi wakuu wa AMECEA waliochaguliwa hivi karibuni katika mkutano wake uliofanyika mjini Lilongwe, Malawi. Mkutano huu unatarajiwa kuhitimishwa hapo tarehe 30 Agosti 2014. Pamoja na mambo mengine, Mama wakuu wa Mashirika ya Kitawa kutoka katika nchi za AMECEA wanajadili kuhusu: mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu, Sheria za Kanisa na Kiraia, Uwazi katika masuala ya uongozi; uwajibikaji; udhibiti wa fedha za Kanisa pamoja na kuandaa bajeti ya Mashirika. Wajumbe pia watasilikiza taarifa ya Shirikisho la Mama wakuu wa Mashirika ya Kitawa Afrika Mashariki na Kati.

Shirikisho hili lilianzishwa kunako mwaka 1974 na kwa sasa linawajumuisha Watawa wa kike wapatao 20, 000. ACWECA pamoja na mambo mengine, linapania kukuza na kuendeleza majiundo makini ya watawa; kuwajengea uwezo watawa ili waweze kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani pamoja na kujitegemea. Ni Shirikisho linalotoa msaada wa kiufundi kwa Mashirika ya Kitawa, ili kweli watawa waweze kuwa ni Mashahidi wa Kristo kati ya watu wanaowahudumia katika sekta mbali mbali za maisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.