2014-08-17 07:54:51

Bwana Lee Ho Jin abatizwa na kuimarishwa kwa Kipaimara na Papa Francisko mjini Seoul!


Baba Mtakatifu Francisko, ameianza siku ya Jumapili tarehe 17 Agosti 2014 kwa kuadhimisha Ibada ambamo ametoa Sakramenti ya Ubatizo, kwa Bwana Lee Ho Jin kwenye Kikanisa cha Ubalozi wa Vatican mjini Seoul, Korea ya Kusini. Huyu ni baba wa mtoto kati ya watoto waliozama na kufa maji kwenye ajali ya Meli iliyotokea Sewol, Korea ya Kusini.

Bwana Lee alionesha nia ya kutaka kubatizwa na Baba Mtakatifu Francisko alipokutana na waathirika wa ajali ya Meli kwenye Uwanja wa Michezo Kimataifa mjini Daejeon. Bwana Lee alitembea umbali wa kilometa tisini kwa mguu aklwa amebeba Msalaba ambao alimkabidhi Baba Mtakatifu Francisko kama kielelezo cha maombolezo yake kutokana na msiba mkubwa uliokuwa umewafika. Katika Ibada hii, Bwana Lee alikuwa ameongozana na watoto wake wawili na Msimamizi wa Ubatizo alikuwa ni mwamini mlei kutoka Ubalozi wa Vatican nchini Korea.

Ibada hii imeadhimishwa katika lugha ya Kikorea na Padre John Chong Che-chon, Myesuit ambaye kwa sasa ni Mkarimani wa Baba Mtakatifu Francisko katika hija yake ya kichungaji nchini Korea. Baba Mtakatifu amembatiza na baadaye kumwimarisha kwa Sakramenti ya Kipaimara na amejichagulia jina la Francisko. Padre Federico Lombardi Msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Baba Mtakatifu amefurahi kuweza kushiriki katika tukio hili la kiimani ambalo halikuwa limepangwa katika hija yake, matendo makuu ya Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.