2014-08-16 15:35:10

Wajibu wa wazazi kwa watoto wao!


Wakati huu Mama Kanisa anapojiandaa kwa ajili ya Maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia sanjari na maadhimisho ya Mwaka wa Familia kwa baadhi ya majimbo nchini Tanzania, Ndugu Antipasi Shinyambala ana machache ya kuishirikisha Familia ya Mungu katika kutambua wajibu wa wazazi kwa watoto wao.

Swali kuu, familia zinaeleza nini kwa watoto? Je, wazazi wana muda wa kukaa, kusali na kula pamoja na watoto wao? Je, wazazi wana muda wa kuwafundisha watoto wao wenyewe juu ya imani na mafundisho tanzu ya Kanisa wanayosimamia na kujitahidi kuyaishi?

"Yesu aliletewa watoto wadogo ili aweke mikono juu yao na kuwaombea; wanafunzi wake wakawakemea. Lakini Yesu akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana waliomfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao. Akaweka mikono yake juu yao, akatoka huko.." (Mt. 19:13-15).

Wanafunzi wa Yesu walitaka kuwazuia watoto wasiende kumpotezea muda Yesu. Mitume walijua kuwa Yesu alikuwa ni kwa ajili ya watu wakubwa tu. Lakini Yesu anatufundisha thamani ya kuwekeza kwa watoto wetu. Hata sisi mara nyingi tunaingia katika mtego huu wa kuwaona watoto hawawezi kujua kitu juu ya ufalme wa Mungu. Tukishawabatiza watoto wetu basi, labda tunaenda nao kanisani kama mazoea tu hatuwafuatilii kama wanacheza au wanasali.

Ni utamaduni au mtindo wa familia nyingi kuwa baada ya kuwabatiza watoto huwa tunawekeza juu ya elimu ya kidunia zaidi na ya kimungu kama ziada. Hatuwekezi sana juu ya elimu ya Mungu hadi wakati wa mafundisho ya komunyo na kipaimara, matokeo yake watoto wetu wanakuwakimwili lakini bila kuwa na misingi bora ya dini. Biblia kwao ni shida wakati masomo ya kidunia, ambayo ni magumu, wanafaulu vizuri sana.

Tunaona hayo ni sawa kwa kuwa hawataajiliwa kwa kigezo cha kujua Biblia au mafundisho ya Mungu. Tunashindwa kuwajenga katika misingi imara ya imani. Watoto wanakuja kusikia kuwa kulipa zaka ni amri, kujenga makanisa ni wajibu wao, wakati wameshajua utamu wa fedha, lazima wajue tu mapadre wa siku hizi wanapenda sana hela na si vinginevyo.


Tukijikita kuwawekea misingi mizuri watoto wetu, wataifuata kwani watoto ni tegemezi, mioyo na akili ya watoto ina nafasi kubwa sana kushika jambo lolote wanalofundishwa na wanaamini kuwa wanachoambiwa na wazazi ni kila kitu. Kazi yetu kwa watoto ni kuamua kuwaunda watoto wetu tunavyotaka, je, tunawapeleka wapi watoto wetu, tunawaruhusu Yesu awafundishe?


Tumuombe Mungu atupe unyenyekevu wa kuwa na akili ya kupokea mafundisho na amri za Mungu kama watoto wadogo, atupe hekima juu ya malezi ya watoto wetu. Tuwaombea watoto wetu ili wakue katika misingi ya hofu ya Mungu ili wawe warithi bora wa imani yetu.
Tumsifu Yesu Kristu!

Ndugu Antipasi Shinyambala.
Dar es Salaam.








All the contents on this site are copyrighted ©.