2014-08-16 12:01:05

Hakuna njia ya mkato katika maisha ya kitawa! Kuna haja ya kujisadaka bila ya kujibakiza!


Mara baada ya chakula cha mchana kilichoandaliwa kwa heshima ya Baba Mtakatifu Francisko na msafara wake, Jumamosi, tarehe 16 Agosti 2014, Baba Mtakatifu alitembelea Kituo cha Afya cha "House of Hope", kilichoko Kkottongnae kinachoendeshwa na Jimbo Katoliki Cheongju.

Askofu Gabriel Bong-hun amemwelezea Baba Mtakatifu tangu kuanzishwa kwa Jimbo hili kunako mwaka 1962, Kanisa limejielekeza zaidi katika kuwahudumia maskini, wagonjwa na wale wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Kituo kinatoa huduma ya elimu kwa watoto walemavu; kuna shule maalum ya watoto wenye ulemavu wa macho, viziwi na walemavu wa viungo. Kunako mwaka 2001 Watawa kwa kusoma alama za nyakati, walianzisha shule kwa ajili ya watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi na wale waliotelekezwa na wazazi wao kutokana na ulemavu.

Mara baada ya kutembelea kituo hiki, Baba Mtakatifu na msafara wake walielekea kwenye kituo cha "School of Love" ili kukutana na Watawa wanaotekeleza utume wao nchini Korea. Baba Mtakatifu katika hotuba yake amekazia kwa namna ya pekee kabisa karama za mashirika ya kitawa na kazi za kitume, utajiri mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa nchini Korea. Huu ni utambulisho kwamba, kweli wanapendwa na Mwenyezi Mungu na kwamba, Mungu ndiye kiini cha wito wao, changamoto ya kujisadaka bila ya kujibakiza kwa ajili ya wengine katika mchakato wa ujenzi wa Ufalme wa Mungu.

Baba Mtakatifu anawataka watawa kuonesha ushuhuda wa huduma inayojikita katika furaha inayobubujika kutoka katika undani wa maisha yao ya kitawa, ili kuwavuta wengine kumfuasa Kristo. Furaha hii inarutubishwa kwa njia ya maisha ya sala, tafakari ya Neno la Mungu, maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa na maisha ya Kijumuiya.

Haya ni maisha yanayofumbatwa katika kazi na tafakari, mambo yanayowasukuma watawa kuwa kweli wataalam waliobobea katika kuwashirikisha wengine huruma ya Mungu kwa njia ya maisha ya kijumuiya. Huu ni mtindo wa maisha ambao unasimikwa katika mashauri ya kiinjili yaani: usafi kamili, ufukara na utii, kielelezo cha furaha ya upendo wa Mungu unaojikita katika mwamba wa huruma. Baba Mtakatifu anawahakikishia watawa kwamba, hapa hakuna njia ya mkato, wanapaswa kweli kujisadaka kwa Mungu bila ya kujibakiza wala kujitafuta wenyewe. Ni mwaliko wa kutoka katika undani wao.

Baba Mtakatifu anawataka watawa kuhakikisha kwamba, wanaonesha ushuhuda wa maisha ya nadhiri ya ufukara katika uhalisia wa maisha yao ya kila siku, katika ngazi ya mtu binafsi na jumuiya katika ujumla wake. Ni wajibu wao msingi kuepuka mambo yote yanayoweza kuwayumbisha na hivyo kusababisha kashfa kwa wengine.

Nadhiri ya ufukara katika maisha ya kitawa anasema Baba Mtakatifu ni ukuta unaolinda maisha ya kitawa na mama anayewasaidia kukua na kutembea katika njia sahihi ya maisha. Watawa hawana budi kuachana na unafiki kuhusiana na nadhiri ya ufukara kwa kuishi maisha ya anasa, jambo linaloharibu Kanisa.

Ni hatari kwa watawa kumezwa na malimwengu, kiasi kwamba huduma wanayoitoa inakuwa kama ile inayotolewa na wafanyakazi wa mshahara kwa kujiamini na kuweka matumaini katika uwezo wao. Mwelekeo wa namna hii unaharibu kabisa ushuhuda wa nadhiri ya ufukara kama ilivyomilishwa katika maisha na kufundishwa na Yesu mwenyewe.

Viongozi wakuu wa Shirikisho la Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume nchini Korea, wamemkaribisha Baba Mtakatifu Francisko na kumshirikisha changamoto wanazokutana nazo katika maisha na utume wao katika ulimwengu mamboleo. Ili watawa waweze kuchuchumilia mafao ya wengi na mafao ya Kanisa, kuna haja ya kutumia karama za mashirika yao pamoja na mapaji ya Roho Mtakatifu, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maisha ya kijumuiya yanayojikita katika hali ya mtu kuwa na kiasi pamoja na kuwashirikisha wengine.

Changamoto kubwa inayowakabili watawa kwa sasa ni kupoteza utambulisho na karama zao, kwa kumezwa na malimwengu badala ya kusoma alama za nyakati kwa njia ya upyaisho wa maisha ya kitawa. Watawa wanaungama yote haya kwa Baba Mtakatifu kwani wanatamani kuwa kweli ni alama ya matumaini kwa njia ya upyaisho wa maisha kuanzia katika ngazi ya mtu binafsi na jumuiya zao za kitawa.

Kanisa Katoliki nchini Korea limerutubishwa kwa njia ya damu na tasaufi ya mashahidi, lakini hata hivyo Jumuiya ya Korea inaendelea pia kuteseka kutokana na athari za utandawazi unaojikita katika ubepari na nguvu ya kisiasa. Kutokana na hali kama hii, Kanisa pia linachangamotishwa kujipyaisha, kwa kuonesha mshikamano wa dhati na watu wanaoteseka, kwa kutambua kwamba, Kanisa linatoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.