2014-08-15 10:28:57

Mama huyu ni kiboko kweli kweli atoa somo!


“Uchungu wa mwana aujuaye ni Mzazi.” Mama mzazi yuko tayari kujitosa ili kumwokoa na kumlinda mwanae mbele ya kila aina ya hatari. Leo tutamwona mama mmoja anayemwingiza Yesu darasani na kumwelewesha jinsi mama anavyoujua uchungu wa kuzaa.

Kituko kizima kilitokea Kanaani, katika nchi ya kipagani ya Tiro na Sidoni ambako Yesu alikutana na huyo mama Mkananayo. Ili kuweza kuupata vizuri ujumbe wa kituko hicho, yabidi tujue kilichomtoa Yesu nchini kwake Uyahudini na kumpeleka nchi hiyo ya watu wa kuja (Wapagani).

Ni kwamba, kabla ya kutoka nchini kwake hali ya hewa haikuwa nzuri kati yake Yesu na mafarisayo na waandishi. Yesu alirushiwa maneno ya kashfa, kwamba hakuwa anawalea vizuri wanafunzi wake jinsi ya kufuata mapokeo ya jadi ya nchi, mathalani juu ya usafi. Yesu naye akawarushia madonge na kuwaambia: “Ninyi ni wanafiki, kwa vile mnajizingizia kufuata mapokeo ambayo mmejitungia wenyewe na kuacha kufuata Neno la Mungu.”

Akawatolea mfano: “Mnajua kuna amri inayosema kwamba yatakiwa kuwatunza wazazi lakini ninyi mwasema, kile kilichotolewa sadaka kwa Mungu ni korbani yaani ni sadaka takatifu, mapato yake hamfanyi chochote.” Baada ya majadiliano hayo, Yesu anawaacha na anarudi nyumbani kwake. Anapofika huko wanafunzi wake wanamtonya: “Unajua mzee, kwamba wafarisayo wamekwazika na kile ulichowazungumzia.” Sasa, kwa vile Yesu alisha chafuka, yaani alishachukizwa na fikra finyu za watu wake, ambazo hata mwenyewe alijisikia amebanwa nazo na zinamkosesha hewa, akaanza kuwapasha wanafunzi wake na kuwaambia hawana akili, akitumia neno kichwa (asunetoi): “Nanyi mnaonekana hamna kitu kabisa kichwani.”

Akaendelea kuwaambia wanafunzi wake: “Ninyi hamwoni kuwa kila kinachomwingia mtu ndiyo kichafu kuliko kile kinachomtoka?” Kutoka hapo anaorodhesha namna saba inayoweza kumfanya mtu awe mchafu moyoni: “mawazo machafu, uuaji, uzinzi, ushahidi wa uwongo, rushwa, nk” kwa hiyo kutawadha peke yake hakutoshi kumsafisha mtu na moyo mchafu wa namna hiyo. Haya ndiyo mazingira yaliyopelekea hadi “Yesu akatoka huko”.

Tendo hilo la “kutoka au kuondoka huko” ni muhimu sana. Hapa umetumika msamiati ule wa kitabu cha Kutoka, kulikowahusu waisraeli walipokuwa bado utumwani Misri. Wakatoka Misri walikokuwa wamefungwa. Walihitaji kutoka na kwenda pahala penye panapowapa uhuru. Ni neno linaloonesha mpito wa kutoka sehemu ya kifungo ambako mtu hawezi kujikamilisha na kujitoshelesha kama binadamu na unashindwa kujibinafasi.

Ieleweke pia kuwa Yesu Mungu nasi amechukua mwili wa binadamu. Alizaliwa, akalelewa na kukua katika mazingira ya fikra na mila za mama wa nchi ya uyahudi. Hivi naye anajisikia kubanwa na fikra finyu za watu wa kabila lake. Hii ndiyo hoja, inayomfanya Yesu aondoke huko aende kwa wapagani akaone kama nao wanafanana na picha ile ya fikra waliyonayo watu wake.

Juu ya huyu mama tungeweza pia kujiuliza: “Hivi huyu ni mama wa namna gani? Halafu tena ni kwa nini afike mama na siyo baba wa mtoto kama ilivyotokea Kafarnaumu kwa yule Senturione aliyefika kumwomba Yesu juu ya mtoto wake?” Jibu ni kwamba mama huyu anaiwakilisha nchi yoyote ile ya kipagani isiyokutana na Kristo. Nchi ya namna hiyo ipo gizani yaani imepagawa na uovu na vurugu za kishetani. Ni ubidamu uliopagawa na shetani anayenyanyasa na kunyima wengine utu wao.

Mama huyu anamkaribia Yesu na kumlilia: “Unirehemu Ee Bwana Mwana wa Daudi, mtoto wangu amepagawa na shetani.” Baada ya ombi hili tungetegemea Yesu anainuka na kwenda mara moja nyumbani kwa mwanamke huyu na kufanya muujiza wa kumfukuza huyo shetani. Kinyume chake, tunavishuhudia vituko ambavyo ni vya muhimu kuvifuatilia. Kituko cha kwanza unamwona Yesu anamchunia mwanamke bila kusema neno lolote. Kituko hiki cha Yesu kumkalia kimya mama huyu kinawakilisha fikra za watu wa kabila lake la wayahudi.

Yaani, tabia ya kutojali shida za watu wasio wa kabila lako na wa dini yako. Yesu anaonekana kuendeleza tabia aliyoirithi dhidi ya wapagani. Ni kweli, mwanzoni mwa shughuli zake Yesu hakushughulika na ulimwengu kijumla kama atakavyosema mwenyewe, kwamba, inabidi ajali zaidi wokovu wa watu wake. Baada ya Yesu kumkalia kimya, kinafuata kituko kingine toka kwa wafuasi wake kinachodhihirisha waziwazi tabia ya kuwatenga wapagani, kwa jinsi wanavyoongea vibaya dhidi yake: “Mfukuzie mbali mama huyu anatupigia-pigia makelele”.

Wanafunzi hawa na mwalimu wao hawakulielewa bado hitaji la ulimwengu wa kipagani juu ya ukombozi utokao kwa Neno la Mungu. Wanataka kumfukuza mama huyu bila hata ya kuhojiana naye na kuelewa dukuduku iliyomo moyoni wake. Baada ya wanafunzi kituko kinachofuata Yesu anazidi kukandamiza zaidi hoja yake anapowaambia wanafunzi: “Mimi sijatumwa isipokuwa kwa kondoo waliopotea wa Israeli.”

Yule mama bila kujali, akaendelea kumpigia Yesu magoti na kumsihi: “Bwana unisaidie”. Hivi ndivyo lilivyo ombi la wapagani la kuomba kupokea Neno la Mungu. Kwa hiyo endapo Uyahudi ni Mama (utu, ubinadamu), hata Upagani ni Mama (utu, ubinadamu) unaohitaji Neno linalofukuza mashetani ya ulimwengu huu wa kipagani, yaani ushetani wa vita, wa uonevu, wa kutesana, wa utumwa, nk. Hapa mwanamke huyu anaelewa fika kwamba, ili kufukuza aina hii ya ushetani unahitaji Neno la mtu kama huyu Yesu wa Nazareti.

Baada ya king’ang’anizi cha mama huyu, kituko kinachofuata Yesu anaamua kumtolea lugha ngumu zaidi mama huyu: “Siyo vyema kuchukua chakula cha watoto na kuwatupia mbwa.” Mbwa anayetajwa hapa ni yule wa kufugwa siyo mbwa koko. Wapagani walieleweka kuwa kama mbwa wa kufugwa. Kwa hiyo, katika nyumba moja watoto hawakutakiwa kula chakula sahani moja na mbwa wa kufugwa.

Na chakula kinachomaanishwa hapa ni Mwanga, ni Neno la wokovu hilo labidi waangaziwe wayahudi tu. Pepo au shetani huyo mchafu anatakiwa atolewe kwa Wayahudi tu. Kwa tamko hilo la Yesu, Mama huyu akatambua kuwa kijana huyu hajakua bado. Kwa sababu Yesu ilimbidi akue katika umri, katika hekima na neema ya kuelewa mpango wa Mungu wa kuukomboa ulimwengu mzima, yaani apanuke katika umisioni ambao ameitwa kuutangaza. Kwa hiyo akiwa kama mama kweli, mwanamke huyu anasimama kidete na kuanza kumsomesha Yesu.

Kwanza anayakubali maneno ya kumlinganisha yeye na mbwa, lakini anaongeza kumwelewesha kwamba “Kwa mbwa vinawatosha vipande vinavyoanguka chini ya meza wanayokula watoto.” Ujumbe huu “Yatosha vipande” ni muhimu sana. Mama huyu anaona kwa ajili ya kuishi watoto wake vinawatosha vipande tu vya chakula anavyowagawia watoto wake (wayahudi -waisraeli).

Jibu hilo ni sawa na alichokisema Yesu mwenyewe kwamba imani ni kama mbegu ya haradali (ndogo sana) lakini inaweza kukua na kufanya muujiza mkubwa. Mwanamke huyu anaelewa kwamba, ili kumponya mtoto, yaani ili kumfukuza pepo huyu anayekandamiza ubinadamu wetu “vinatosha vipande” tu. Jibu la mama huyu linamtoa Yesu kutoka kwenye fikra finyu za kiyahudi alizokulia nazo. Yesu anafunguka akili na angeweza tu kusema “mama ujumbe nimeupata” badala yake anaishia tu kushangaa na kumwambia mwanamke yule: “imani yako ni kubwa, utendewe kama unavyotaka”.

Yesu anashangaa kuona jinsi binadamu wa ulimwengu wa kipagani walivyo na imani kuu kwa Neno lake kwamba lina uwezo wa kufukuza aina zote za pepo. Ukuu wa imani ya mama huyu upo katika kuamini kwamba Mungu ni kama mama aliye na uchungu na watoto wake. Mama huyu hana imani kali ya kitaalamu, bali ana imani ya mama mwenye uchungu na watoto wake.

Anamfahamu kwa undani Mungu kuwa yu kama mama na anaungana naye katika moyo wake wa umama. Yaani ni Mungu anayeonja maumivu ya vidonda vya waana wake. Ama kweli “Uchungu wa mwana aujuaye mzazi”. Na Mungu ndiye mzazi mkuu. Mungu aliye mama anafurahi anapomwona mama yeyote mwenye furaha. Mungu ana uchungu anapomwona mama yeyote kuwa na uchungu kwa mtoto wake. Mama huyu anasadiki kwamba haki kuu mbele ya Mungu ipo katika kuteseka na mwenye kuteseka. Haki hiyo ni kwa ajili ya watoto wote wa Mungu, iwe watoto wa wayahudi, watoto wa wakanaani, watoto walio ndani ya kanisa au nje ya kanisa, watoto walio bara au walio visiwani.

“Imani yako ni kubwa” hayo ni maneno sahihi kabisa katika ulimwengu wa leo. Imani namna hiyo haina dini wala utaifa. Kuna wamama wengi kama huyu mkananayo ambao hawajui kusali kanisani wala kuswali msikitini, lakini wanaujua moyo wa kimama alio nao Mungu. Wako wamama wengi leo wasiolijua jina la Mungu, bali wanajua kwamba Mungu anao moyo wa kimama. Huyo mama Mungu ni wa sisi watoto wake wote tunaoteseka ulimwenguni.

Kwa hiyo ujumbe tunaopata leo ni huu kwamba, ulimwengu unasubiri Neno linalouponya kutokana na kila aina ya ushetani unaomnyima utu binadamu. Na Neno hilo ni Yesu mwenyewe. Kinatosha kipande kidogo tu cha imani kwa Yesu ili kuweza kutenda muujiza.Yesu anatualika sisi leo tuwe kama yeye, yaani tuwe na uchungu kwa jamii zetu kama “mama alivyo na uchungu kwa mwana wake”. Uchungu wa kuiona njaa ya watoto (jamii) na kuituliza.

Ujumbe mwingine ni kwamba Yesu anatoka, anatembea na kukua katika imani, anajifungua kwa mkananayo wa Tiro na Sidoni, na hivi "anabangatuliwa" akili na mwanamke huyu mpagani. Anatufundisha kutambua kwamba binadamu mwenye hekima ni yule aliye kama Yesu anayetoka na kwenda kujifunza toka kwa kila mtu. Nasi tuwe na hekima kama ya Yesu ya kuwa tayari kutoka na kwenda kujifunza toka kwa kila mtu hata yule tunayemdhani kuwa ni mchovu.

Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.