2014-08-15 12:16:24

Changamoto za maisha ya ujana!


Askofu Lazzaro You Heung-sik wa Jimbo Katoliki la Daejeon, Mwenyeji wa maadhimisho ya Siku ya Sita ya Vijana Barani Asia, akimkaribisha Baba Mtakatifu Francisko kwenye Madhabahu ya Solmoe anasema, ni furaha kuu isiyokuwa na kifani kuwakaribisha wageni waliofika kutoka mbali, lakini kwa namna ya pekee Baba Mtakatifu Francisko.

Madhabahu ya Solmoe ni mahali alipozaliwa Mtakatifu Andrea Kim Daegeon, Padre wa kwanza wa Kanisa Katoliki nchini Korea, aliyezaliwa na kukumbatia imani bila ya uwepo wa Wamissionari, mfano wa pekee kabisa duniani! Hapa ni mahali ambapo mashahidi wengi wa imani wameteswa na kuuwawa kikatili, ni watu walioonesha ushuhuda wa imani katika matendo.

Kongamano la Sita la Vijana Barani Asia ni changamoto ya kichungaji kwa Wakristo na Wakatoliki kwa namna ya pekee kabisa kwani Kanisa linakabiliwa na changamoto mbali mbali katika maisha na utume wake. Uchu wa mali na utajiri wa haraka haraka ni mambo yanayopelekea kumong'onyoka kwa tunu msingi za maisha ya kimaadili na utu wema na mateokeo yake ni watu kukumbatia utamaduni wa kifo na uharibifu wa mazingira.

Hii ndiyo changamoto kwa Wakristo kuwa kweli ni mashahidi kwa kuchagua na kukumbatia ukweli unaomwilishwa katika uhalisia wa maisha, ili kushinda vishawishi vinavyowazunguka. Wakristo kwa kufuata mfano wa mashahidi na mwanga wa Injili wanapaswa kuwasha mwanga wa imani kwa kufanya maamuzi ya maisha na kuyatolea ushuhuda kwa kujikita katika imani thabiti kama walivyofanya Mashahidi wa Korea waliojisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, huku wakipambana na ukanimungu, utamaduni wa kifo, uchu wa mali na madaraka.

Askofu Lazzaro You Heung-sik anahitimisha hotuba yake ya makaribisho kwa Baba Mtakatifu kwa kumwomba asonge mbele ili kuinjilisha Ulimwengu na Kanisa, wao wako nyuma yake na wana muunga mkono.

Baba Mtakatifu kwa umakini mkubwa amesikiliza shuhuda ambazo zimetolewa na vijana Cambodia, Hong Kong na Korea waliomshirikisha kuhusu ndoto za maisha yao wakitaka kuwa Mapadre ili kujitosa kimasomaso kwa ajili ya kuwatangazia watu Injili ya Furaha, lakini bado hawana msingi thabiti wa imani. Vijana wanakabiliana na changamoto nyingi za kiimani, kimaadili na utu wema. Kuna baadhi ya nchi hazina uhuru wa kidini, Je, kama vijana wajibu na utume wao ni nini?

Kanisa lina watakatifu lakini pia limejaa wadhambi, zote hizi ni changamoto za maisha, ili kutubu na kuongoka, ili kuonja huruma, msamaha na upendo wa Mungu. Vijana wengi wanaonekana kana kwamba, wamechanganyikiwa kutokana na kumezwa mno na malimwengu, kinzani pamoja na kujisikia kuwa ni wanyonge. Yote haya yanapelekea kuongezeka kwa uhalifu na vijana kujinyonga; kwa ufupi vijana wengi wamechanganyikiwa kiasi cha kukosa utambuzi wa tunu msingi katika maisha chemchemi ya furaha ya kweli. Korea bado imegawanyika, watu wanaishi katika chuki na uhasama. Hizi ni baadhi ya changamoto wanazokabiliana nazo vijana Barani Asia.







All the contents on this site are copyrighted ©.