Maaskofu wanachangamotishwa kuwa ni walinzi wa kumbu kumbu na matumaini!
Baba Mtakatifu Francisko akizungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Korea amekazia
kuhusu mambo makuu mawili yaani kama Maaskofu wamepewa dhamana ya kulinda kundi la
Kristo katika kumbu kumbu na matumaini, kwa kutambua kwamba, wao ni kizazi na urithi
wa kishujaa ulioneshwa katika imani kwa Kristo, utume ambao umefanywa kwa umakini
mkubwa na waamini walei.
Kanisa nchini Korea ni matunda ya watu kukutana moja
kwa moja na Neno la Mungu, ambalo limemwilishwa katika maisha na vipaumbele vya waamini.
Ni Neno ambalo limechochea wongofu wa ndani na upyaisho wa maisha unaojikita katika
mapendo, kama ilivyooneshwa na wazee wa kizazi kilichotangulia.
Haya ni matunda
ya uhai wa Kanisa unaojionesha katika Parokia, Vyama vya kitume, malezi kwa vijana
wa kizazi kipya shuleni, seminarini na katika vyuo vikuu ambamo Katekesi makini inakaziwa
kwa namna ya pekee. Kanisa nchini Korea linaheshimiwa sana kutokana na utume wake
katika maisha ya watu kiroho, kitamaduni pamoja na mwamko na ari ya kimissionari.
Baba
Mtakatifu anawataka Maaskofu kuwa ni walinzi wa hazina kubwa ya neema waliyoipokea;
kutumia rasilimali ya maisha ya kiroho ili kukabiliana kwa mwono mpana na matumaini
makubwa ahadi na changamoto zijazo. Maisha na utume wa Kanisa nchini Korea unapimwa
mintarafu Mwanga wa Injili na mwaliko wa kumwongokea Yesu Kristo kwa kutambua kwamba,
Mwenyezi Mungu ndiye anayewezesha ukuaji makini wa mwamini.
Haya ni matunda
ya uvumilivu na udumifu katika kazi kama ilivyojionesha siku za nyuma na kama ilivyo
kwa sasa. Kumbu kumbu endelevu ya mashahidi wa imani haina budi kuonesha ukweli na
wala si kielelezo cha ushindi. Waamini waangalie historia yao na wawe tayari kumsikiliza
Mwenyezi Mungu, ili kujikita katika hija ya maendeleo ya maisha ya kiroho.
Maaskofu
wanaalikwa kwa namna ya pekee kuwa ni walinzi wa matumaini yanayobubujika kutoka katika
Injili na neema pamoja na huruma ya Mungu kwa njia ya Yesu Kristo. Hii ni changamoto
kwa waamini kuwatangazia walimwengu hazina kubwa na ya kweli inayompatia mwanadamu
ukamilifu wa maisha. Matumaini haya yanaweza kulindwa kwa kuendelea kuwasha moto wa
utakatifu wa maisha, upendo wa kidugu, ari ya kimissionari na umoja wa Kanisa.
Baba
Mtakatifu Francisko anawataka Maaskofu Katoliki nchini Korea kujenga Kanisa la Kimissionari
ambalo liko tayari kutoka kwenye pembezoni mwa jamii mamboleo ili kujenga vionjo vya
maisha ya kiroho, vinavyowawezesha waamini kujitambulisha kuwa ni sehemu ya Fumbo
la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa. Kipaumbele cha pekee, kitolewe kwa watoto pamoja
na kuzima kiu ya matamanio ya vijana, kwa kuwaenzi wazee ambao ni hazina ya hekima
na mang'amuzi.
Kama walinzi wa matumaini wanapaswa kuonesha ushuhuda wa kinabii
kwa kujenga mshikamano wa upendo na udugu kwa wakimbizi, wahamiaji na wote wale wanaosukumizwa
pembezoni mwa jamii. Kanisa lijikite katika mchakato wa maendeleo endelevu katika
jamii, ili kutengeneza fursa za ajira na nafasi za elimu. Huduma za kijamii zinazotolewa
na Mama Kanisa ziwasaidie watu kukua na kukomaa kama binadamu, ili kumwezesha mtu
kuonesha utu wake, ugunduzi na utamaduni.
Hapa kuna haja ya kukuza na kujenga
dhana ya Kanisa maskini kwa ajili ya maskini, kama ilivyokuwa kwa Wakristo wa Kanisa
la mwanzo. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, dhana hii ya Kanisa la
Mwanzo itaendelea kuliunda Kanisa la Korea kwa siku za usoni.
Baba Mtakatifu
anakumbusha kwamba, ushuhuda wa Kiinjili unachangamoto zake hususan kwa Kanisa nchini
Korea, mahali ambapo Kanisa linaishi na kutekeleza utume wake miongoni mwa watu wenye
uwezo lakini wako kwenye hatari ya kumezwa mno na malimwengu.
Kutokana na
mwelekeo kama huu, viongozi wa Kanisa wanapaswa kuwa makini kwa kuchagua mtindo wa
kuratibu, kupanga na kutumia mali ya dunia hii. Ni watu wanaopaswa kuwa pia na mtindo
wa maisha unaowawezesha kutomezwa na malimwengu, uchu wa mali na madaraka, bali kwa
kujikita katika kanuni msingi za Injili ya Kristo.