Lengo la hija ya kitume ni: kushiriki maadhimisho ya Siku ya VI ya Vijana Barani Asia
na Kuwatangaza Watumishi wa Mungu 124 kuwa Wenyeheri!
Baba Mtakatifu Francisko kabla ya kuzungumza na viongozi wa serikali nchini Korea
na Mabalozi wanaowakilisha nchini zao, amemtembelea Rais wa Korea ya Kusini Bibi Park
Geunhye katika Ikulu yake inayojulikana kama "Blue House". Nyimbo za nchi hizi mbili
zimepigwa na hatimaye, Baba Mtakatifu Francisko akakagua gwaride la heshima na baadaye
viongozi hawa wawili wamefanya mazngumzo ya faragha pamoja na kubadilishana zawadi.
Baba
Mtakatifu Francisko katika hotuba yake kwa viongozi wa Serikali ya Korea ya Kusini
amegusia malengo makuu mawili, yaani kushiriki katika maadhimisho ya Siku ya VI ya
Vijana Barani Asia, hii ni sherehe ya imani inayowaunganisha vijana wakatoliki kutoka
nchi mbali mbali Barani Asia. Lengo la pili ni kuwatangaza Watumishi wa Mungu 124
kutoka Korea kuwa ni Wenyeheri. Hawa si wengine bali ni Paul Yun Jichung na wenzake
123.
Baba Mtakatifu anawapongeza wananchi wa Korea kwa kuwathamini wazee kwa
kuwaenzi na kuwashirikisha katika maisha ya kijamii. Ni jamii inayopenda na kuheshimu
mapokeo yake pamoja na kuwathamini vijana, ili kuwarithisha tunu msingi za maisha
ya kijamii ili kuwajengea uwezo wa kukabiliana na changamoto za nyakati hizi. Baba
Mtakatifu anawaalika kwa namna ya pekee wananchi wa Korea kutafakari kwa makini namna
bora zaidi ya kurithisha tunu msingi za maisha ya kijamii, ili kuunda jamii wanayokusudia.
Baba
Mtakatifu katika hotuba yake anagusia pia: amani, upatanisho na utulivu nchini Korea
na kwamba, hii ni changamoto kubwa na endelevu kwa wanadiplomasia kuhakikisha kwamba,
wanavunja kuta za utengano na chuki, ili kujenga utamaduni wa upatanisho na mshikamano
wa dhati; mambo msingi yanayopaswa kupewa kipaumbele cha pekee.
Amani anasema
Baba Mtakatifu, si ukosefu wa vita na kinzani bali ni kazi ya haki inayojikita katika
msingi wa kuheshimiana, kuelewana na upatanisho. Uzoefu katika ulimwengu wa utandawazi
unawataka watu kufahamiana, ili kutafuta mafao ya wengi na maendeleo ambayo yanapaswa
kuzingatia mahitaji ya mtu mzima: kiuchumi na kiutu.
Baba Mtakatifu anasema
katika mchakato wa maendeleo, nchi zilizoendelea duniani zinakabiliana na matatizo
na changamoto nyingi za kijamii, migawanyiko ya kisiasa, ukosefu wa usawa kiuchumi
pamoja na kuwa na matumizi sahihi na yanayowajibisha kutunza mazingira.
Baba
Mtakatifu anawahimiza viongozi nchini Korea kujitahidi kujenga utamaduni wa kusikilizana
katika ukweli na uwazi; kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa jamii; kwa watu wasiokuwa na sauti pamoja na kuwasaidia kupata mahitaji
yao msingi, ili kushiriki kikamilifu katika mchakato wa ukuaji wao kiroho na kiutu.
Baba
Mtakatifu kwa mara nyingine tena anakazia utamaduni wa utandawazi unaojikita katika
mshikamano, ukiwa na lengo la kukoleza maendeleo ya kila mwanafamilia ya binadamu.
Baba Mtakatifu anasema, ni hamu ya Jumuiya ya Waamini wa Kanisa Katoliki nchini Korea
kushiriki kikamilifu katika maisha ya taifa lao.
Kanisa linapenda kuchangia
katika sekta ya elimu kwa vijana, ukuaji wa ari na moyo wa mshikamano kwa maskini
na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; majiundo makini kwa vijana wa kizazi kipya,
ili waweze kuwa ni raia wema kwa kuwarithisha hekima na busara kutoka kwa mababu zao
na katika imani, ili kukabiliana na changamoto za kisiasa na kijamii zinazojitokeza
nchini mwao.