Kardinali Braz de Aviz, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi
za Kitume hivi karibuni akizungumza na wakuu wa Mashirika ya kitawa na kazi za kitume
mjini Melbourne, nchini Australia amewataka watawa kujenga na kudumisha mahusiano
yanayojikita katika vinasaba vinavyodhihirisha kwamba, Mungu ni upendo.
Wakuu wa
Mashirika ya kitawa na kazi za kitume, walikuwa wanafanya mkutano wao mkuu uliokuwa
unaongozwa na kauli mbiu “ Kuishi changamoto wadau katika hali ya mabadiliko”.
Kardinali
Braz anasema, leo hii haitoshi kuwa na kanuni maadili, urithi wa maisha ya kiroho
kutoka kwa waanzilishi wa mashirika ya kitawa na kazi za kitume au sera na mikakati
ya kichungaji inayowawezesha watawa kutangaza kwa ari na moyo mkuu Habari Njema ya
Wokovu inayojikita katika ushuhuda wa maisha ya Kikristo. Kumbe, kuna haja kuonesha
ushuhuda wa maisha ya kitawa unaojikita katika maisha ya pamoja yanayokuza na kudumisha
tasaufi ya umoja, upendo na mshikamano, mambo msingi aliyokazia Mtakatifu Yohane Paulo
II kama nguvu ya Kanisa, katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Watawa
wanapaswa kujibu changamoto zinazojitokeza katika maisha na utume wao katika ulimwengu
wa maendeleo ya sayansi na teknolojia kwa kujikita katika utekelezaji wa mwaliko unaotolewa
na Baba Mtakatifu Francisko kwa watawa kuhakikisha kwamba, wanauamsha ulimwengu, na
huu ukawa ni mwanzo wa cheche za maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani.
Kardinali
Braz anasema, nyakati hizi kuna maendeleo makubwa ya sayansi na teknolojia, mambo
ambayo yamelea mabadiliko makubwa katika maisha ya mwanadamu katika medani mbali mbali
za maisha. Mahusiano na mwingiliano kati ya watu ni mambo yanayokwenda kwa haraka
na kwa nguvu ya ajabu hata na wale ambao wako mbali kabisa.
Leo hii maendeleo
ya mitandao ya kijamii yanawawezesha watu kupata habari za haraka kutoka sehemu mbali
mbali za dunia, kiasi kwamba, ulimwengu mamboleo umekuwa kama kijiji! Watu wanaweza
kusafiri kwenda sehemu mbali mbali za dunia kwa kutumia muda kidogo, yote haya yanaonesha
jinsi ambavyo utandawazi ulivyokuwa na kukomaa.
Lakini, changamoto kubwa kwa
sasa ni kuona kwamba, zile tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kitamaduni zilizowaunganisha
watu kutoka kila kabila, lugha, jamaa na taifa zinawekwa pembeni kana kwamba, zimepitwa
na wakati. Hizi ni tunu msingi za maisha ya mwanadamu zilizojenga na kukuza mahusiano
kati ya mwanadamu na Muumba wake na kati ya binadamu wenyewe, leo hii, ubinafsi, dhana
ya mawazo mepesi mepesi na watu kumezwa na malimwengu, ni mambo yanayoendelea kumkoroga
mwanadamu.
Bila uwepo wa Mwenyezi Mungu, Sheria na Kanuni maadili, kila mtu
anakuwa ni hakimu wa mawazo na matendo yake; anakuwa na uwezo wa kujitafuta mwenyewe
na kuambatana na mambo yanayompatia furaha hata kama ni furaha ya mpito. Tunu msingi
za maisha na ukweli wa binadamu zinawekwa rehani, kiasi cha kuvuruga mahusiano kati
ya watu.
Kardinali Braz anasema, kwa mtindo na mwelekeo huu wa mawazo, nadhiri
ya utii, ufukara na usafi kamili zinaonekana kuwa ni mambo ya kale, yaliyopitwa na
wakati, eti watu wanapaswa kuponda mali, kufa kwaja! Hapa umuhimu wa maisha ya pamoja,
unaangaliwa kwa jicho la kengeza, kwani kwa hapa wanasema, maisha ya kijumuiya ni
mateso makubwa kwa mtawa.
Ukweli huu unajionesha hata miongoni mwa watawa
walioweka nadhiri za daima na wale ambao wameanza kuchungulia tu maisha ya kitawa
kwa kutaka kuachana kidogo na maisha haya, ili waonje kile ambacho wamekikosa huko
duniani, kwa maneno mengine ni watu wanaotaka kuonja uhuru binafsi na wasipokuwa makini,
huko wanajichumia majanga!
Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi
za Kitume linasema, sababu kubwa inayotolewa na watawa wanaotaka kuacha maisha ya
kitawa si kwamba, walikosea kuchagua wito, bali ni kutokana na hali ya kutosikia tena
Jumuiya yao ya kitawa kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi, hapa Jumuiya imekuwa
kama ni gereza dogo, mahali ambapo mtu anashindwa kujiamria mambo yake mwenyewe, kimsingi,
watawa hawajisikii kamwe kwamba, wana ile furaha waliyokuwa nayo siku ile walipokuwa
wanapigiwa vigelegele na kuvikwa mashada ya maua kwa kuweka nadhiri zao za daima!
Hali na mwelekeo huu ni changamoto kubwa kwa watawa na inahitaji watawa wenyewe
kujenga na kuimarisha mahusiano yao yanayojikita kwa kutambua kwamba Mungu ni upendo
n ani chanzo mshikamano wa upendo kati ya watu wanaotoka katika kila kabila, lugha
na jamaa. Ni watu ambao wamekombolewa kwa Damu ya Mwanakondoo wa Mungu.
Imehaririwa
na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.