2014-08-13 12:32:32

Kituo cha Radio Kabangabanga Zambia chazinduliwa rasmi!


Askofu mkuu Julio Murat, Balozi wa Vatican nchini Zambia, hivi karibuni alizindua Kituo Kipya cha Radio Katoliki Kabangabanga, kilichopo Jimboni Solwezi, Zambia. Askofu Charles Kasonde wa Jimbo Katoliki Solwezi ndiye aliyebariki kituo hiki ambacho kinakuwa ni kituo cha tisa cha Radio zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki nchini Zambia.

Serikali ya Zambia imelipongeza Kanisa kwa kuanzisha kituo cha radio na kuwataka kuhakikisha kwamba, wanatengeneza vipindi kadiri ya mahitaji ya wananchi wa Zambia, hasa kwa kujikita katika tunu msingi za maisha ya kifamilia, maadili na utu wema, mambo ambayo yanapaswa kupewa kipaumbele cha pekee katika tasnia ya habari.

Takwimu zinaonesha kwamba, walau kila Jimbo Katoliki nchini Zambia, limebahatika kuwa na Kituo cha Radio kama sehemu za utekelezaji wa mikakati yake ya shughuli za kichungaji, zinazopania Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima kwa kutimia njia za mawasiliano ya kisasa. Itakumbukwa kwamba, kuibuka na kuenea kwa Vituo vya Radio vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki ni matunda ya maadhimisho ya Awamu ya kwanza ya Sinodi ya Maaskofu wa Bara la Afrika, iliyofanyika mjini Vatican kunako mwaka 1994.

Hadi sasa nchini Zambia, kuna vituo viwili vya radio ambavyo vinafanyiwa kazi kwa sasa navyo ni Radio Lutanda kilichoko Jimbo kuu la Kasama na Kituo cha radio Sesheke, kitakachokuwa Magharibi wa Jimbo la Sesheke.







All the contents on this site are copyrighted ©.