2014-08-13 10:37:57

Kanisa lina matumaini makubwa kwa Bara la Asia!


Baba Mtakatifu Francisko anapoianza hija yake ya kitume nchini Korea ya Kusini inayoongozwa na kauli mbiu "Ondoka, uangaze, kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa Bwana umekuzukia" anawaalika Waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuungana naye kwa njia ya sala ili kuiombea Korea na Asia katika ujumla wake.

Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican anasema hija ya kitume ya Baba Mtakatifu ina umuhimu wake kwa maisha na utume wa Kanisa Barani Asia. Kwa mara ya kwanza, Baba Mtakatifu anafanya hija ya kitume Korea ya Kusini, lakini akiwa na mwelekeo kwa Kanisa zima Barani Asia, kwani Baba Mtakatifu atashiriki katika maadhimisho ya Siku ya Sika ya Vijana Barani Asia.

Lakini, ikumbukwe kwamba, Bara la Asia linaendelea kuimarika katika masuala ya kisiasa na kiuchumi. Baba Mtakatifu anapenda kuwekeza kwa vijana Barani Asia, ili waweze kuwajibika barabara katika maisha na utume wa Kanisa. Vijana wanapaswa kuwa ni Wainjilishaji miongoni mwa vijana wenzao, kwa kujikita katika majiundo makini yanayozingatia ukuaji wa mtu mzima: kiroho na kimwili.

Baba Mtakatifu akiwa nchini Korea anatarajia kuwatangaza Wafiadini 124 kutoka Korea ya Kusini kuwa ni Wenyeheri. Hili kundi kubwa la waamini walei na kati yao kuna Padre mmoja tu; waamini ambao walijisadaka kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa nchini Korea, changamoto kwa waamini walei kuwa kweli ni mashahidi wa imani kwa Kristo na Kanisa lake. Wakristo wanahamasishwa kuwa ni watangazaji wa Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya ushuhuda wa maisha; kwa kuchuchumilia utakatifu wa maisha kadiri ya wito na nafasi ya kila mwamini.

Akiwa nchini Korea, Baba Mtakatifu atakutana na kuzungumza na watu walioguswa na ajali ya kuzama kwa Meli huko Sewol, na kusababisha watu 300 kupoteza maisha yao. Hii ni ajali ambayo imewagawa wananchi wa Korea ya Kusini. Baba Mtakatifu anataka kuonesha jinsi ya kuponya madonda ya ndani, kwa kuwa karibu na wote walioguswa na ajali hii mbaya; hiki ni kielelezo cha imani na upendo.

Kardinali Parolin anasema, Baba Mtakatifu Francisko atahitimisha hija yake ya kitume kwa kusali kwa ajili ya kuombea amani na upatanisho kati ya Korea ya Kusini na Korea ya Kaskazini, kwani Korea bado inaendelea kuteseka kutokana na uwepo wa vita baridi, ambayo kwa sasa haina tena mashiko wala mafao kwa ustawi na maendeleo ya watu. Vatican inapenda kushiriki katika mchakato wa majadiliano, ili kujenga na kuimarisha upatanisho na umoja wa kitaifa.







All the contents on this site are copyrighted ©.