Barua ya Papa kwa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Iraq
Baba Mtakatifu Francisko amemwandikia ujumbe maalum Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa
Bwana Ban Ki-Moon kumwelezea hofu na mashaka yake kuhusu mateso na mahangaiko ya watu
wasiokuwa na hatia Kaskazini mwa Iraq, wengi wao wakiwa ni Wakristo wamelazimika kuyakimbia
makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha yao. Kumekuwepo na uharibifu mkubwa wa nyumba
za ibada na urithi wa kidini.
Kwa kusukumwa na mateso ya watu hawa, Baba Mtakatifu
anasema amemtuma kama mjumbe wake maalum nchini Iraq, Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti
wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu ambaye aliwahi kuwa Balozi wa Vatican
nchini Iraq, ili kuonesha mshikamano wake wa dhati na Kanisa zima, kwa watu wanaotaka
kuishi kwa amani, utulivu na uhuru katika ardhi ya Mababu zao.
Baba Mtakatifu
anasema, anamwandikia ujumbe huu Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, akiweka mbele yake
machozi, mahangaiko na hali ya kukata tamaa inayooneshwa na Wakristo pamoja na makundi
madogo madogo ya kidini nchini Iraq. Anaiomba Jumuiya ya Kimataifa kuchukua hatua
madhubuti ili kukomesha majanga haya.
Baba Mtakatifu anayahimiza Mashirika
ya Kimataifa hususan yanayojihusisha na masuala ya usalama, amani, sheria na huduma
kwa wakimbizi, kuendeleza juhudi zao kadiri ya Sheria za Umoja wa Mataifa. Mateso
na mahangaiko ya watu wasiokuwa na hatia Kaskazini mwa Iraq yaamshe dhamiri nyofu
kwa watu wenye mapenzi mema ili kuonesha mshikamano wa upendo kwa kuwalinda waathirika
pamoja na kuwapatia msaada wanaohitaji wale wote wasiokuwa na makazi maalum kwa wakati
huu pamoja na kuhakikisha kwamba, wanafanikiwa kurudi katika makazi yao salama salimini.
Kuna
haja ya kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu, kwa kuzingatia sheria za
kimataifa pamoja na Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, inaweka mikakati makini
itakayozuia mauaji yanayojikita katika ukabila na udini. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu
Francisko na Wakuu wa Makanisa ya Mashariki pamoja na viongozi mbali mbali kwamba,
ujumbe wake utapata jibu makini kutoka katika Umoja wa Mataifa.