2014-08-12 11:54:57

Ninyi ni chumvi na mwanga wa dunia!


Baba Mtakatifu Francisko anawapongeza Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanaojisadaka kwa ajili ya kuwasaidia maskini, wakati huu, Baraza la Maaskofu Katoliki Argentina linapoadhimisha Siku ya 45 ya Sadaka kwa ajili ya Maskini, linaloongozwa na kauli mbiu "Asante kwa msaada wako".

Baba Mtakatifu katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican kwenda kwa Askofu Adolfo Armando Uriona, Mwenyekiti wa Tume ya Baraza la Maaskofu Katoliki Argentina kwa ajili ya msaada kwa maeneo yenye uhitaji zaidi, anawatia shime waamini kuonesha imani yao kwa njia ya matendo ya kawaida kwa kutokumbatia mno malimwengu, ili kuonesha mshikamano wa upendo, ili waendelee kuwa kweli ni chumvi na mwanga wa dunia kwa njia ya imani tendaji; upendo wa kidugu na mshikamano wa dhati kwa maskini wanaoonesha ile sura ya Kristo!

Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuendelea kumsindikiza katika maisha na utume wake kwa njia ya sala na kwamba, anawaweka wote chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria Mama yetu wa Lujan, ili tukio hili la mshikamano liweze kuzaa matunda yanayokusudiwa!







All the contents on this site are copyrighted ©.