2014-08-11 09:51:27

Licha ya mawimbi mazito, lakini imani kwa Kristo inaweza kuwaokoa waja wake!


Baba Mtakatifu Francisko, wakati wa tafakari yake ya Injili ya Jumapili ya kumi na tisa ya kipindi cha Mwaka wa Kanisa, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 10 Agosti 2014 amefafanua kuhusu muujiza wa Yesu kutembea juu ya bahari baada ya kufanya muujiza wa kuwalisha watu elfu tano kwa mikate mitano na samaki wawili.

Mitume walipomwona Yesu anatembea juu ya bahari walishikwa na woga, lakini Yesu mwenyewe aliwatuliza. Kama ilivyo kawaida ya Mtakatifu Petro, akataka kuhakikisha kweli kwamba, alikuwa ni Yesu, akamwomba ili yeye pia aweze kutembea juu ya bahari. Yesu akamkaribisha na Petro akaanza kutembea juu ya bahari, lakini alipoona upepo mkali akaanza kuzama na hatimaye akampigia kelele Yesu ili aweze kumwokoa.

Papa Francisko anasema, Mtakatifu Petro aliitambua sauti ya Kristo, akajiachilia mikononi mwa Yesu ambaye ni Mwalimu na Bwana akamfuata. Mtakatifu Petro alianza kuzama pale alipoonesha mashaka, lakini Yesu yuko daima tayari kuwaokoa wale wanaomkimbilia.

Huyu ndiye Mtume Petro anayeonesha ukakamavu na mapungufu yake, kielelezo cha imani ya Wakristo ambayo daima inaonesha umaskini, lakini yenye nguvu ya kupata ushindi; hii ni imani ya Mkristo anayetembea ili kukutana na Yesu Kristo mfufuka, kati ya mawimbi mazito na hatari za maisha.

Baba Mtakatifu anasema, Yesu alipopanda kwenye mashua mambo yote yakawa shwari, kiasi cha Mitume wote kumwabudu Yesu kuwa ni Mwana wa Mungu. Ndani ya mashua kuna Mitume wenye uzoefu na mang'amuzi ya mapungufu yao ya kibinadamu, wasi wasi na mashaka, lakini kwa pamoja wanajisikia wamoja katika imani wakimzunguka Yesu Kristo. Bila kuwa karibu na Yesu, daima wafuasi wake watajisikia waoga, kwani hiki ni kielelezo cha ukosefu wa imani, lakini Yesu yuko tayari kuwaokoa waja wake wanapomlilia kwa imani na matumaini.

Hii ndiyo sura ya Kanisa ambalo halina budi kukabiliana na changamoto mbali mbali za maisha, lakini waamini wanaweza kuokolewa ikiwa tu watakuwa na imani thabiti, inayowawezesha kutembea hata katika giza na uvuli wa mauti bila ya kuogopa. Imani inawahakikishia waamini uwepo endelevu wa Kristo katika maisha yao. Waamini wanaweza kujisikia kuwa salama pale tu wanapopiga magoti ili kumwabudu Mwana wa Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.