Mchango wa Kanisa Katoliki Tanzania katika sekta ya elimu!
Askofu John Ndimbo, Mwenyekiti wa Idara ya Elimu, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania
katika mahojiano maalum na Radio vatican anabainisha mchango wa Kanisa Katoliki katika
sekta ya elimu, mafanikio na changamoto wanazokabiliana nazo, ili kuhakikisha kwamba,
elimu inasaidia kumpatia mwanadamu ukombozi wa kweli, kiroho na kimwili, kama sehemu
ya mwendelezo wa mchakato wa utume ulioanzishwa na Yesu, Mwalimu na Mponyaji!
Kanisa Katoliki
Tanzania kwa sasa linaundwa na majimbo 34 na walau kila Parokia imebahatika kuwa na
shule ya awali na kwamba, Kanisa linamiliki na kuendesha shule za msingi 100, Sekondari
220, zikiwemo Seminari 37 kwa ajili ya majiundo makini ya Makasisi kwa siku za usoni.
Shule hizi zinamilikiwa na kuendeshwa na Majimbo pamoja na Mashirika ya Kitawa na
Kazi za Kitume yanayotekeleza dhamana na wajibu wake nchini Tanzania.
Kanisa
Katoliki nchini Tanzania linaendesha vyuo vya ufundi stadi 75 ambavyo vimesajiliwa
na VETA. Hapa wanafunzi ambao hawakubahatika kuendelea na masomo ya sekondari wanapatiwa
mafunzo ya taaluma, ili kuweza kujiajiri mara tu wanapohitimu masomo yao. Kanisa pia
linamiliki na kuendesha vyuo vikuu viwili: Chuo kikuu cha Mtakatifu Agostino cha Tanzania,
SAUT pamoja na Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Afya na Sayansi Mwambata, Bugando, CUHAS,
bila kusahau matawi ya vyuo kumi ya vyuo hivi yaliyoenea sehemu mbali mbali za Tanzania.
Askofu
Ndimbo anasema kwamba, Kanisa Katoliki Tanzania limepata mafanikio makubwa kwenye
sekta ya elimu kutokana na ubora, umakini wa elimu inayotolewa katika vyuo vinavyomilikiwa
na kuendeshwa na Kanisa Katoliki kwa kuzingatia viwango vya elimu. Matunda yake yanaonekana
katika soko la ajira ndani na nje ya Tanzania.
Pamoja na mafanikio yote haya,
Askofu Ndimbo kwa unyenyekevu mkubwa anakiri kwamba, taasisi za elimu zinazomilikiwa
na kuongozwa na Kanisa Katoliki Tanzania bado zina uwezo mdogo ikilinganishwa na hitaji
la wanafunzi wanaoomba kujiunga na vyuo hivi. Baadhi ya shule zinatoza ada kubwa na
hivyo familia za maskini na watu wa kawaida wanashindwa kufaidika na huduma ya elimu
inayotolewa na Kanisa.
Kuna mwelekeo mkubwa kwa mashirika mengi ya kitawa
kutaka kujenga shule na taasisi za elimu mijini, hali inayoonesha kwamba, kama hakuna
mikakati ya makusudi, huduma ya elimu inayotolewa na Kanisa Katoliki vijijini inaweza
kuathirika vibaya, hapa kinachotafutwa ni soko!
Askofu Ndimbo anasema, Kanisa
bado linakabiliwa na uhaba wa nguvu kazi na rasilimali watu ili kuendesha taasisi
za elimu nchini Tanzania na kwamba, bado kuna taasisi za elimu zinazoendeshwa kimapokeo,
mwelekeo ambao umepitwa na wakati, kiasi cha kusababisha weledi kuwa hafifu, kuna
haja kwa Kanisa kuwekeza katika majiundo ya rasilimali watu, ili kuendeleza mbele
mafanikio yaliyokwishakupatikana katika sekta ya elimu nchini Tanzania. Kuna haja
pia ya kuwa na uhakika wa rasilimali fedha kwa kujijengea misingi ya kujitegemea.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.