Kardinali Filoni, kumwakilisha Papa Francisko nchini Iraq, ili kuonesha mshikamano
wake wa dhati!
Baba Mtakatifu Francisko, huku akiwa ameguswa kwa namna ya pekee kabisa na mahangaiko
pamoja na mateso ya Wakristo pamoja na watu mbali mbali wanaolazimika kuyakimbia makazi
yao huko Iraq kutokana na madhulumu, vita na nyanyaso za kidini, amemteua Kardinali
Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu kumwakilisha
nchini Iraq, kama kielelezo cha mshikamano wa dhati katika maisha ya kiroho na Wakristo
pamoja na wote wanaoteseka nchini Iraq kutokana na vita inayoendelea huko.
Huu
ni mshikamano wa Mama Kanisa na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na
imani yao kwa Kristo na Kanisa lake au kutokana na sababu mbali mbali! Kardinali Filoni
anasema kwamba, Baba Mtakatifu ameonesha imani kwake binafsi, lakini zaidi anaguswa
na mahangaiko ya wananchi wa Iraq ambao kwa sasa wanakabiliwa na hali ngumu sana ya
maisha kutokana na vita inayoendelea nchini humo.
Watu wengi wamelazimika
kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha yao na kwa sasa wanaishi kama
wakimbizi hata katika nchi yao wenyewe. Kardinali Filoni anasema, akiwa nchini Iraq
atazungumza na viongozi wa Makanisa, ili kuangalia ni mambo yepi wanayoweza kutenda
kwa pamoja. Hali ni ngumu hata namna ya kufika nchini humo, lakini hakuna sababu ya
kuwa na woga wala wasiwasi, Kanisa litafanya kile kinachowezekana.
Kardinali
Filoni anasema, hii si mara ya kwanza kwa Wakristo nchini Iraq kulazimika kuyakimbia
makazi yao. Mateso na mahangaiko ya Wakristo huko Iraq yanafahamika kihistoria na
kwamba, hii ni Jumuiya ambayo imeendelea kubeba ndani mwake Msalaba na kuifuata ile
Njia ya Msalaba.
Hija yake nchini Iraq anasema Kardinali Filoni inapania kuonesha
mshikamano wa Baba Mtakatifu Franciko kwa Wakristo huko Iraq, ambaye anaendelea kuwasindikiza
katika mateso na mahangaiko yao kwa njia ya sala na sadaka yake takatifu. Kardinali
Filoni anasema, atawasilisha ujumbe wa Baba Mtakatifu kwa Wakristo wa Iraq.
Baba
Mtakatifu Francisko amemteua Kardinali Filoni kutokana na uzoefu wake mkubwa huko
Mashariki ya Kati, kwani amewahi kuwa Balozi wa Vatican nchini Jordan na Iraq kwa
muda wa miaka saba. Ni kiongozi aliyeonja adha ya vita wakati wa utawala wa Rais Saddam
Hussein, lakini akabaki, akiwa ameshikamana kwa dhati na wananchi wa Iraq katika kipindi
hiki kigumu.