2014-08-08 09:47:27

Changamoto katika utoaji wa huduma za kijamii nchini Tanzania


Askofu Severine Niwemugizi wa Jimbo Katoliki Rulenge - Ngara ambaye pia ni Makamu wa Rais, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, huduma za kijamii zinazotolewa na Kanisa ni sehemu ya mchakato wake wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. RealAudioMP3

Lakini ikumbukwe kwamba, serikali inawajibika kutoka huduma za kijamii kwa ajili ya watu wake. Kumbe, Kanisa linachangia katika maboresho ya huduma za kijamii nchini Tanzania. Ili kutekeleza azma hii kuna haja ya kuimarisha ushirikiano zaidi kati ya Kanisa na Serikali. Dhana ya kwamba, Kanisa linafaidika sana kutokana na huduma inazotoa katika sekta ya jamii ni kikwazo kikubwa cha ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa katika kuwahudumia watanzania.

Askofu Niwemugizi anasema kwamba, Kanisa inakabiliwa na changamoto mbali mbali, ikiwepo uhaba wa rasilimali fedha kwa ajili ya kuendeshea taasisi zake za afya. Hapa Serikali katika sera yake ya ushirikiano na taasisi binafsi ilikwisha sema kwamba, itasaidia kulipia mishahara ya wafanyakazi wa sekta ya afya wenye taaluma na viwango vinavyotakiwa, lakini hata hili utekelezaji wake bado unasuasua kwa kiasi kikubwa!

Askofu Niwemugizi anabainisha kwamba, Makanisa na Halmashauri yalianza mchakatato wa majaribio ya mikataba mipya, lakini hata hapa bado utekelezaji wake bado ni kidogo sana, kiasi cha kukwamisha jitihada za Kanisa katika kushiriki kwenye mchakato wa maboresho ya maisha ya watanzania kwa kuchangia katika utoaji wa huduma za kijamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.