2014-08-06 12:06:24

Shirika la Masista wa Mtakatifu Yosefu Jimbo kuu la Mombasa lapata "Majembe mapya"


Askofu Emmanuel Barbara wa Jimbo Katoliki Malindi ambaye pia ni msimamizi wa kitume wa Jimbo kuu la Mombasa, katika Ibada ya Misa Takatifu kabla ya uchaguzi mkuu wa Shirika la Masista wa Mtakatifu Yosefu, Jimbo kuu la Mombasa, amewaambia Watawa hao kwamba, Mwenyezi Mungu huchagua viongozi sio kwa sababu ya uwezo wao wa kiakili au nguvu walizo nazo, bali ni kwa sababu anataka kuwaimarisha na kuwatumia kama vyombo vya kueneza utukufu wake.

Viongozi wanaochaguliwa kuwaongoza watawa wenzao wanakumbushwa kwamba, wanaitwa kuwa wahudumu, wanaopaswa kusaidiana kwa kuoshana miguu kama alivyofanya Yesu mwenyewe kwa wanafunzi wake. Hii ni changamoto ya kutoa huduma makini na yenye tija kwa Watu wa Mungu bila kubagua, kama anavyojitahidi kufanya Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wake. Viongozi wawe ni mfano wa unyenyekevu, walezi wema, wapole na watakatifu, ili kuwasaidia watawa wenzao kuishi kweli za Kiinjili kwa kuendeleza maisha ya kitawa, tayari kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa.

Wajumbe wa mkutano mkuu wa Shirika la Masista wa Mtakatifu Yosefu Jimbo kuu la Mombasa wamemchagua Sr. Jane Irene Awuor kuwa Mama mkuu wa Shirika na Msaidizi wake ni Sr. Elizabeth Nduku. Washauri wakuu wa Shirika ni Sr. Terezia Waweru, Sr. Betty Shao pamoja na Sr. Bridgita Mwawasi.

Askofu Emmanuel Barbara amewataka viongozi wapya kutekeleza dhamana na wajibu wao kikamilifu wakitambua kwamba, wanafanya dhamana hii kwa niaba ya Shirika. Kumbe, wanapaswa kumtegemea Mwenyezi Mungu, ili aweze kuwaongoza daima, kama alivyofanya kwa Waisraeli walipokuwa wanaelekea kwenye Nchi ya ahadi, iliyojaa maziwa na asali.

Askofu Barbara amewashukuru watawa kwa huduma bora wanazotoa kwa ajili ya Familia ya Mungu ndani na nje ya Bara la Afrika, hasa kwa kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Masista hawa wameombwa kumwangalia Mtakatifu Yosefu, aliyeonesha utii na unyenyekevu katika kutekeleza mpango wa Mungu katika maisha yake, akawa Baba mlishi na mwema kwa Mtoto Yesu. Huu ni mwaliko kwa Watawa kuandamana na Yesu katika kutangaza Injili ya Furaha kwani Yeye ndiye sababu ya wito na maisha yao ya kitawa!







All the contents on this site are copyrighted ©.