2014-08-06 09:48:03

Papa Paulo VI na Kanisa la Kristo!


Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI mara tu baada ya kuchaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki tarehe 21 Juni 1963, kunako tarehe 10 Agosti 1964, Papa Paulo VI akachapisha Waraka wake wa kwanza wa kichungaji, unaojulikana kama "Ecclesiam Suam" "Kanisa la Bwana", Waraka unaonesha dira na mwelekeo wa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo, kwa kuzingatia changamoto zilizotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Ni katika mwelekeo huu, Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI akafanya hija ya kitume Nchi Takatifu ili kukutana na kusali na Patriaki Anathegoras, mwanzo wa mchakato wa majadiliano ya kiekumene kati ya Makanisa. Papa Paulo VI katika Waraka huu analitaka Kanisa kutambua dhamana na wajibu wake; kuanza mchakato wa kujipyaisha kwa kujielekeza katika majadiliano ya kidini na kiekumene, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI anapenda kuwaambia watu wa mataifa kwamba, Kanisa limebarikiwa kuwa na amana ambayo watu wanaitafuta katika historia ya maisha yao. Ni Waraka unaojikita katika fadhila ya mapendo kwa Mungu na jirani. Ni kutokana na mwelekeo huu, Kanisa halina budi kuwashirikisha watu upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Watu watambue kwamba, Kristo ndiye ile hazina iliyofichika machoni pa wengi, lakini ni muhimu sana katika maisha ya watu.

Tafakari ya kina iliyofanywa na Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI, ilihitimishwa tarehe 11 Julai 1964. Kuanzia tarehe 6 Agosti 1964 alianza utume wake mjini Vatican, wakati Mama Kanisa alipokuwa anaadhimisha Siku kuu ya Kung'ara kwa Bwana, kielelezo cha ufunuo wa Mungu na utukufu wa Kristo, ili kuwaimarisha Mitume wake waweze kukabiliana barabara na Kashfa ya Msalaba. Miaka kumi na minne baadaye, Papa Paulo VI tarehe 6 Agosti 1978, akiwa Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo, akafariki dunia, huku akiwa anasali, ile sala kuu, yaani Sala ya Baba Yetu.







All the contents on this site are copyrighted ©.