2014-08-06 09:15:46

Papa Francisko ni mjumbe wa upatanisho!


Kardinali Andrew Yeom Soo-jung, Askofu mkuu wa Jimbo kuu Seoul, Korea ya Kusini anasema, hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Korea ya Kusini kuanzia tarehe 13 hadi tarehe 18 Agosti 2014 kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya sita ya vijana wa Bara la Asia ni tukio la aina yake kwa wananchi wote wa Korea. RealAudioMP3

Ni matumaini ya Kanisa nchini Korea kwamba, Baba Mtakatifu Francisko atasaidia mchakato wa kuziunganisha Korea ya Kusini na Korea ya Kaskazini; nchi pacha ambazo kwa zaidi ya miaka hamsini zimekuwa zikiangaliana kwa “macho ya makengeza”.

Kardinali Andrew anasikitika kusema kwamba, kukosekana kwa majadiliano ya kina kati ya Korea ya Kusini na Korea ya Kaskazini ni mambo ambayo yanatishia amani, usalama na ustawi wa wananchi wa pande hizi mbili, ambao kimsingi wanapaswa kuwa kweli ni wamoja. Hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Korea, inaweza kuwa ni mwanzo mpya wa mchakato wa majadiliano na upatanisho kati ya Nchi hizi mbili.

Hii inatokana na ukweli kwamba, Baba Mtakatifu Francisko ni kiongozi anayependa kuona haki na amani vikitawala, sanjari na utunzaji bora wa mazingira pamoja na kutetea utu na heshima ya binadamu. Haya ni mambo msingi ambayo ameyaonesha tangu awali kabisa alipochagulia kuliongoza Kanisa Katoliki. Haki na amani, utu na heshima ya binadamu ni dhana inayomwilishwa katika uhalisia wa maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko kama ilivyojionesha wakati wa hija yake ya kitume katika Nchi Takatifu.

Wananchi wa Korea wanaweza hata wao kuishi katika umoja na udugu. Licha ya kinzani zinazoendelea huko Mashariki ya Kati, lakini Baba Mtakatifu Francisko hapo tarehe 8 Juni 2014 aliweza kuwakutanisha Marais wa Palestina na Israeli mjini Vatican ili kusali kwa ajili ya kuombea amani huko Mashariki ya Kati. Hii ni mbegu ya amani iliyopandwa katika mioyo ya watu, itazaa matunda kwa wakati wake.

Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Francisko hapo tarehe 18 Agosti 2014 kabla ya kukunja vilago na kurejea tena mjini Vatican ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuombea amani na upatanisho nchini Korea. Tarehe 10 Agosti 2014 mjini Geneva, Baraza la Makanisa Ulimwenguni limeandaa Ibada maalum ya kiekumene kwa ajili ya kuombea amani na upatanisho kati ya Korea ya Kusini na Kaskazini.








All the contents on this site are copyrighted ©.