2014-08-06 14:53:07

Papa aendelea na Katekesi yake kwa mahujaji na wageni.


Jumatano hii, Baba Mtakatifu Francisko, alianza tena kutoa katekesi kwa mahujaji na wageni, hapa Vatican licha ya kuwa kipindi cha mapumziko katika kipindi cha joto kali.Papa akiwa tofauti na watangulizi wake , ameamua kubaki katika makazi yake ya Vatican badala ya kwenda nje ya Vatican.

Katekesi yake ya Jumatano hii, iliendelea kutoa tafakari juu Kanisa, Taifa la Mungu. Alisema, Kanisa likiwa limeandaliwa tangu katika Agano la Kale na kujengwa na Kristo katika utimilifu wa wakati, Kanisa linakuwa ni watu wapya, waliojengwa katika Agano Jipya.

Papa Francisco amefafanua kwamba, upya unaoletwa na Kristo, hauweki kando kile kilichoandaliwa kabla, , lakini hukamilisha yaliyoandaliwa. Katika maandiko, Matakatifu Yohana Mbatizaji, ni kiungo kati ya ahadi na unabii wa Agano la Kale na utimilifu wao katika Agano Jipya. Yohana anasema, aliendelea kueleza Papa, kwamba, anamtaja Yesu na kututaka sisi tumfuate, kwa kufanya toba na kubadilika. Na sheria mpya ambayo Yesu anatoa katika Hotuba ya Mlimani , ilikamilisha sheria aliyopewa Musa juu ya Mlima Sinai.

Yesu katika hotuba yake ya Heri aliyoitoa milimani , anatuonyesha njia ambayo, pamoja na neema yake, tunaweza kufikia furaha halisi. Anatuambia, katika Injili ya Mathayo, kwamba maisha yetu ya Kikristo yatahukumiwa kwa jinsi gani tulimtendea yeye kupitia watu wadogo na hasa watu waliotupwa pembezoni na jamii na watu maskini wahitaji.

Na kwamba katika moyo wa agano jipya, tunapata kutambua kwamba, ndani ya Kristo , tunakumbatiwa na neema na huruma ya Mungu, na kwamba maisha yetu lazima yaonyeshe ushuhuda wa upendo wake alioutoa kwa watu wote wake kwa waume.

Kama kawaida Papa baada ya kukamilisha Katekesi yake alisalimia makundi mbalimbali ya watu waliofika kumsikiliza . Katika katekesi hii kulikuwa na makundi makubwa ya watu Uingereza, Norway, Zimbabwe, Japan na Marekani. Na kwao wote aliwapa baraka zake kwao na familia zao akiwaombea furaha na amani katika Bwana Yesu.









All the contents on this site are copyrighted ©.