2014-08-06 15:02:42

Kanisa laomba siku tatu za toba na mafungo kupambana na ebola


Katika kikao maalum kilichojumuisha viongozi wa Makanisa nchini Liberia, Maaskofu Katoliki , Wachungaji na wakuu wa makanisa mengine mbalimbali, kwa lengo la kujadili jinsi ya kupambana na virusi vya ebola vilivyotia hofu kubwa raia wa Liberia,viongozi hao wanasema, jibu la kwanza kwanza kabisa ni kumlilia Mungu mwenye uweza wa kusitisha uwepo wa virusi hivyo vinavyokatisha maisha ya watu bila huruma. Kwa ajili hiyo Kanisa limetoa wito kwa watu wote, kuwa na siku tatu za mafungo na toba kama hatua ya kupambana na ebola.

Kikao hicho kilifanyika chini ya uenyekiti wa Rais wa Baraza la viongozi wa Kidini uliofanyika hapo tarehe 30 Julai 2014, katika Kanisa la Kiinjili la Mtakatifu Stephano, kilihudhuriwa na viongozi wa Kanisa kutoka pande zote za Liberia. Katika kikao hicho , Viongozi hao walipendekeza siku hizo tatu za mafungo na toba zianze Jumatano hii tarehe 6 Agosti hadi Ijumaa ijayo , watu wabaki majumbani mwao kusali na kufunga , kumlilia Mungu kwa bidii, aliepushe taifa lao na janga hili la ebola. Uwe ni wakati pia wa kuwaombea baraka na usalama wafanyakazi wote wa afya wanaohudumia wagonjwa wa ebola kwa wakati huu.









All the contents on this site are copyrighted ©.