2014-08-04 09:56:35

Papa asema kuweni watu wa huruma, ushirikiano na shukurani..


Jumapili wakati wa sala ya Malaika wa Bwana, Papa Francisco akiuhutubia makusanyiko ya watu katika uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, alielekeza mawazo katika somo la Injili, juu ya mikate na samaki kama ilivyoandikwa katika Injili ya Mathayo (14:13-21), muujiza wa Bwana Yesu, kulisha watu ya elfu tano kwa mikate mitano na samaki wawili.

Papa Francisko, alisema somo hili lina mambo matatu muhimu katika maisha ya kila Mkristo nayo ni: huruma; kushirikiana; shukrani, ambavyo ni kiini cha Sakramenti ya Ekaristi. "Kristo" alisema Papa Francisko, hakughadhabishwa na umati wa watu, waliokuwa wakimfuata, kila mahali kwa bidii, bali aliwahurumia kwa sababu Alijua kwamba, hawamfuati tu kwa sababu za udadisi, lakini walikuwa na haja. Papa Francisko aliendelea kusema kwamba, uponyaji mwingi wa Kristo, ulifanywa kwa ishara ya huruma yake. Kwa mifano hiyo Yesu anatufundisha kujali mahitaji ya watu wahitaji na hasa maskini wetu wenyewe. Mahitaji yetu, hata kama ni halali, kamwe si ya dharura, kama ya wenzetu maskini, ambao wanakosa mahitaji muhimu katika maisha.

Akiligeukia kugawana mkate , Papa Francisko, alilinganisha majibu ya wanafunzi wakati wanakabiliwa na watu wengi wahitaji, na jibu la Yesu. Wanafunzi wanaona ni halali kuwaambia watu waondoke waende kujitafutia kwingine chakula, lakini Yesu anawaambia, waliulishe umati wa watu huo kwa chakula walichokuwa nacho. Katika hili Papa alieleza, tunaona mambo mawili , wanafunzi wanafikiri na kutoa jibu kwa mtazamo wa kidunia, ambamo kila mmoja na ajitunze mwenyewe, Na Yesu anatoa jibu katika mantiki ya Kimungu, ambayo ni ile ya kugawana kilichopo. Na hivyo kwa Mantiki ya Kimungu watu walikula hadi kutosheka na kusaza. Hii ilikuwa ni ishara inayotualika tujenge imani kwa Mungu. Na kwamba Mungu wa huruma, hatulazimishi sisi kwenda nje kutafuta mkate wetu wa kila siku, iwapo tunajua jinsi ya kugawana na ndugu zetu wake kwa waume wahitaji, kile tulicho nacho.

Na tatu katika ujumbe wake, Papa alizungumzia juu ya ekaristi, ujumbe unaosikika wakati Yesu akiubariki Mkate kuugawa katika umati wa watu . Inasemekana ni tendo hilohilo alilolifanya katika karamu yake ya mwisho, wakati alipoweka kumbukumbu ya kudumu ya sadaka yake ya ukombozi, kumbukumbu kwamba, si mkate wa hapa duniani, lakini mkate wa uzima wa milele, zawadi ya Kristo ya Nafsi yake, anaitoa Yeye mwenyewe kwa Baba kwa upendo kwa ajili yetu.


Papa Francisko alihitimisha kwa sala ya Mama yetu, Mama wa Maongozi ya Mungu, ili aweze kuongozana na sisi katika hija yetu ya kidunia na atusaidie sisi katika jitihada za kukidhi mahitaji ya wale tunao kutana nao njiani katika roho ya udugu.







All the contents on this site are copyrighted ©.