2014-08-04 09:39:11

Kiburi ni kaburi la utu na heshima ya binadamu!


Mpendwa msilikilizaji wa kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo! Karibu katika kipindi chetu tuendelee kuitafakari familia kama shule ya fadhili na maadili. Katika vipindi vilivyopita, tulijaribu kuitazama fadhila ya unyenyekevu na umuhimu wake katika jamii ya watu. Tulihitimisha vipindi vyetu kwa kualikana kuwa tuwe wanyenyekevu katika yote, na kwa njia hiyo tutainuliwa katika yote na tutajenga amani na wenzetu. RealAudioMP3

Tunakamilisha somo letu lile kwa kutafakari kilema ambacho kinapingana moja kwa moja na fadhila ya unyenyekevu, nacho si kingine bali ni kiburi. Kiburi ni hali ya kujiona na kujidhani kuwa umekamilika katika yote na juu ya yote, na hivyo huhitaji neno wala chochote kutoka kwa yoyote.

Kilema cha kiburi huendana na tabia za majivuno, kujikweza, kujisifu, ukaidi, kujiamini kupita kiasi, maringo na dharau. Pamoja nazo kinaambatana pia na tabia za kutoambilika, kutoulizika, kutoshaurika na kutoonyeka. Kiburi ni kilema kibaya sana kwa sababu ndiyo kinachotutenga na wanadamu wenzetu na mwisho kinatutenga na Mungu. Mbaya zaidi, huweza pia kubadili hulka yetu kama asemavyo Mt. Augustino, “kiburi kiliwafanya malaika wakawa mashetani”. Na sisi tuwapo na kiburi huwa tunakuwa ni shetani na ndiyo maana katika kiburi twafanya mambo mengi ya kishetani-shetani.

Watu wenye kiburi wanatazamwa na maandiko matakatifu kama ishara pia ya mwisho wa nyakati. Mwisho wa nyakati uliyojaa uangamizi huashiriwa na jinsi watu walivyo na kiburi. Neno linasema “...katika siku za mwisho...watatokea watu wasio na upendo mioyoni, wasio na huruma, wachongezi, walafi na wakali..., wakaidi na waliojaa kiburi” (rej. 2Tim 3:1-9). Kiburi ni ishara ya uangamizi na maandiko yanaonesha wazi, mwisho wa mwenye kiburi sio mwema; na hata historia zinatushuhudia pia, wenye kiburi wote waliangukia pua. Mkumbuke Sauli mfalme, kwa kiburi chake aliifukuza neema ya Mungu na Bwana akamkataa. Badala ya kumtegemea Mungu, kiburi chake kilimtuma awategemee wachawi. (1Nyakt.10:13-14a).

Kiburi na mtu wa kiburi ni chukizo kwa Bwana. Maandiko yasema “kuna vitu sita anavyovichukia Bwana, naam vipo saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi mdanganyifu, mikono imwagayo damu, moyo uwazao mawazo mabaya, miguu myepesi kukimbilia maovu, shahidi wa uwongo abubujikaye uwongo na mtu apandaye mbegu ya fitina kati ya ndugu” (Mith. 6:16-19). Hapo tunaona wazi msululu wote wa machukizo huo hutoka kwa mtu mwenye kiburi. Mtu mwenye kiburi kwa kiburi chake yupo tayari kutenda kila aina ya dhambi ndiyo maana mafundisho ya imani yetu, yanatuelekeza kwamba kiburi ni moja ya mizizi ya dhambi.

Rai tunayoitoa hapa kwa wazazi na wote wenye dhamana ya malezi katika familia ya mwanadamu ni kwamba, tujitahidi kuwalea watoto wetu katika fadhila njema, na kuwasaidia wasikomae katika kiburi, kwani kiburi huwapeleka kuishi katika utundu wenye kifo ndani mwake. Watoto wetu wajengwe katika usikivu na utii kwa wazazi, walimu, walezi na wote wenye mamlaka halali. Hizi fujo nyingi za vijana zinazosikika mashuleni hata maofisini, zina msingi katika kiburi tunachokomaa nacho tangu udogoni.

Yoshua Bin Sira anatuonya sana juu ya madhara ubaya wa kiburi na matokeo yake. Nasi katika tafakari hii, tunataka tutumie kitabu cha Yoshua Bin Sira kama dira yetu. Mintarafu kiburi, Yoshua Bin Sira anatuasa “mwenye kiburi ataishia vibaya mwishoni...atalemewa na taabu” (rej. YbS. 3:26-27). Na haswa wengi huwa tunakuwa watu wema kwa nyakati fulani, lakini pale tunapoingiliwa na kiburi, basi mwisho huwa unakuwa ni wa aibu. Ili kutuangusha kwa kutuporomosha kwa aibu na fedheha, shetani hutuinua juu kwa kutujaza kiburi kikavu kisichorekebishika isipokuwa kwa anguko kuu la aibu.

Kiburi huwafanya wenye akili waonekane hawana maarifa tena. Historia zinatushuhudia kwamba, wapo watu wengi, waliokuwa watawala na enzi na mamlaka, walianza kwa uungwana, lakini kwa sababu ya kiburi chao wakaifukuza neema ya Mungu, mwishoni wakawa chukizo kwa wote.

Daima na popote, kiburi hubeba mimba ya uharibifu na aibu. Hakuna mwenye kiburi anayeweza kusimama siku zote. Mwenye kiburi lazima ataangushwa tu, na anguko lake huwa ni la aibu kuu. Sote daima tunapoiambata fadhila ya unyenyekevu, tuombe neema ya kuepukana na kiburi. Kilema cha kiburi hutufanya tuchukiwe na watu na tupoteze maana katika jamii tunamoishi. Kiburi sio uungwana!

Kutoka katika studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.