2014-08-04 10:53:37

Dini lisiwe ni jukwaa la kuwagawa wananchi kwa mafao ya kisiasa!


Askofu Emmanuel Badejo wa Jimbo Katoliki la Oyo, nchini Nigeria, amewataka wanasiasa nchini Nigeria kuacha mtindo wa kutumia dini kama jukwaa la kutekeleza matakwa yao ya kisiasa na matokeo yake wanasababisha kinzani za kidini na migawanyiko ya kijamii! Uchu wa mali na madaraka na ubinafsi ni kati ya mambo ambayo yameendelea kusababisha majanga makubwa kwa nchi nyingi Barani Afrika.

Pale ambapo wanasiasa wametumia dini kama jukwaa la utekelezaji wa utashi wao wa kisiasa, hapo kumekuwepo na kinzani pamoja na machafuko ya kidini. Hali kama hii ndiyo inayoendelea kujitokeza nchini Nigeria. Tofauti za kidini na kiimani ni utajiri mkubwa unaoweza kutumiwa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya nchi husika na kamwe, kisiwe ni chanzo cha kinzani, migongano na hatimaye vita ya kidini, jambo ambalo kwa sasa limepitwa na wakati.

Askofu Badejo anasema, wanasiasa wengi nchini Nigeria wameanza kujipanga kwa ajili ya kuanza mchakato wa uchaguzi mkuu nchini humo, unaotarajiwa kufanyika kunako mwaka 2015. Mashambulizi ya kigaidi yanayoendelea kufanywa na Kikundi cha Boko Haram sehemu mbali mbali za Nigeria na kushindwa kwa Serikali kuweza kukidhibiti ni kielelezo wazi kwamba, hapa si bure, kuna mkono wa baadhi ya wanasiasa ambao wanaunga mkono vitendo vinavyofanywa na Boko Haram kwa ajili ya mafao yao binafsi.

Inasikitisha kuona kwamba, Nigeria, iliunda mazingira na hatimaye kuibuka kwa Kikundi cha Boko Haram na sasa Nigeria si mahali pa amani na utulivu tena, kwani watu wanaishi kwa wasi wasi mkubwa kuhusu maisha na mali yao!







All the contents on this site are copyrighted ©.