Chama cha Wanataaluma wa Kikristo Tanzania, CPT, hivi karibuni kiliviandikia vyama
vya kisiasa nchini Tanzania ujumbe maalum kuhusiana na Bunge maalum la Katiba, kuhusu
kuwaangusha watanzania katika mchakato wa Bunge hili, umuhimu wa kujikita katika misingi
sahihi ya kisheria pamoja na kuhakikisha kwamba muafaka unafikiwa, ili watanzania
waweze kupata Katiba mpya. Kwa undani zaidi endelea kujichotea changamoto hii.
Waheshimiwa
Viongozi wa Vyama vya Siasa Tanzania, kwa heshima na upendo, tunawatumia kwa njia
ya Ujumbe huu salaam za Mshikamano, Maridhiano na Amani! Katika Ujumbe wetu huu kwenu,
tumezingatia “Ujumbe wa Kichungaji wa Pasaka 2014 kwa Waamini na watu wote wenye mapenzi
mema” uliotolewa mwezi Aprili na Maaskofu Katoliki 32.
Tunasukumwa na moyo
wa Mshikamano, Maridhiano, na Umoja wa Taifa letu Tanzania na watu wake kwa misingi
ya Uhuru, Ukweli, Uwazi na Haki, inayozaa Uvumilivu na Amani ya kweli. Tunaomba na
kuasa kuwa Ujumbe wetu huu upokelewe, kama ulivyonuiwa, kama mwaliko wa kuwa na moyo
wa kujenga imani, si wa kukatisha tamaa na kutapanya viongozi na watu wote wenye nia
na mapenzi mema kwa Wananchi na Nchi yetu Tanzania.
UJUMBE Katika Bunge
Maalumu la Katiba mmewaangusha Wananchi
Watu wamechoka na mambo mengi
yanayoendelea nchini. Tunahisi wanasema: ‘Yatosha’! Wazo la Katiba Mpya linachukuliwa
kama nyenzo; watu wameiona kama njia au nyenzo ya kufikia upatikanaji wa mabadiliko
wanayoyatamani. Maoni ya Wananchi yaliyokusanywa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (Tume ya Warioba) hadharani na kwa njia za wazi yaliwaamsha
watu kuhusu dhima yao katika utawala wa Nchi na uundwaji wa Katiba yake.
Walitoa
maoni yao wakiwa huru kwa namna na katika njia na majukwaa huru mbalimbali; na walitegemea
yabainishwe katika Taarifa na Rasimu ya Katiba rasmi ya Tume ya Warioba. Taarifa na
Rasimu rasmi ya Tume ya Warioba vimezingatia kwa kiwango kikubwa maoni yaliyotolewa
na Wananchi na kukusanywa na Tume hiyo.
Hata hivyo, hadi sasa, ahadi, iliyo
katika Taarifa na Rasimu ya Tume ya Warioba, iko njia panda na imekwama.. Imekwamishwa
na wanasiasa katika Bunge Maalumu la Katiba na mtuhumiwa mkuu ni Chama Tawala ambacho,
kwa makusudi, kimekataa kuipa Rasimu rasmi ya Katiba hadhi yake stahiki kwa mujibu
wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya Mwaka wa 2011 kama ilivyofanyiwa mabadiliko hadi
2013, kifungu cha 25. Masharti ya Kifungu hicho, katika kifungu kidogo cha (2) yanasema
kama ifuatavyo: (2) Mamlaka ya Bunge Maalum ya kupitisha masharti ya Katiba inayopendekezwa
yatatekelezwa baada ya Rasimu ya Katiba kuwasilishwa na Mwenyekiti wa Tume na kupitishwa
na Bunge Maalum. Hii inamaanisha na kunuia kwamba (isipokuwa kwa tafsiri tofauti
ya mahakama yenye mamlaka), ili “Bunge Maalum kupitisha masharti ya Katiba inayopendekezwa”
itazingatia Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya
Katiba na si Rasimu nyingineyo yoyote.
Pasipo shaka, Rasimu ya Tume ya Warioba
inaweza kuboreshwa na Bunge Maalum kwa masharti yake kufafanuliwa, kupanuliwa upeo
au wigo wake, kuyaimarisha na kuyatengamaza lakini bila kutoka nje ya misingi yake,
tunu na nguzo zake za kimsingi zinazotokana na kuaswa kwa kiwango kikubwa na ”’maoni
ya wananchi” kwa madhumuni ya kutunga Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano.” (Kifungu
cha 3 cha Sheria hiyo.)
Tunahitaji kuanzia kwenye misingi sahihi
Je,
watu wanataka nini? Wanataka kuwa wamoja, wenye heshima na wanaothaminiana, kila mmoja
akiwa na thamani yake katika jamii. Msingi wetu wa kina ni utu na tunu za maadili. Rasimu
ya II ya Tume ya Warioba inauwasilisha vyema msingi huu.
Yabidi
juhudi ya kuweka msingi huu ifanywe kidhati katika Bunge Maalum la Katiba
Majadiliano
yawe huru, yasibanwe na misimamo ya vyama vya siasa. Vyama vya siasa, ambavyo ni makundi
madogo kati ya jamii kubwa zaidi ya Wananchi, viwape wajumbe na wafuasi wao maagizo
ya kufuata maoni binafsi ya moyoni na akili zao katika kujadili mawazo, maoni na mapendekezo
ya Wananchi yaliyo katika Rasimu ya Tume ya Warioba iliyowasilishwa rasmi na Mwenyekiti
wa Tume hiyo kwenye Bunge hilo. Muache kufanya siasa za kivyama kwenye Bunge Maalum
la Katiba. Muikubali Rasimu rasmi ya Tume ya Warioba kama inavyotakiwa na sheria kama
msingi halali wa kutafuta muafaka wa kitaifa katika Bunge Maalum hilo.
Rasimu
hiyo imewasilishwa kwa wananchi na Rais mwenyewe kwa Taarifa yake (Rais) : Toleo hili
la Rasimu ya Katiba linachapishwa kwenye Gazeti la Serikali kwa mujibu wa kifungu
cha 20(2) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura ya 83, na itawasilishwa kwenye
Bunge Maalum la Katiba kwa ajili ya kujadiliwa na kupitishwa. Dar es Salaam Jakaya
Mrisho Kikwete22 Januari, 2014 Rais
Mh. Rais anawajibika kushauri Bunge Maalum
na kuomba radhi Mh. Rais anawajibika kulishauri Bunge Maalum hilo kufuata njia
hii; pia anapaswa kuomba radhi kwa kuondoa mchakato kwenye misingi na njia yake rasmi
iliyowekwa kisheria.
Hatua za kisheria dhidi ya Bunge Maalum?
Kama
haya tunayoasa na kushauri hayawezi kupatikana kihiari, itabidi hatua za kisheria
zichukuliwe dhidi ya Bunge Maalum la Katiba, au kuomba mahakama yenye mamlaka kutoa
tafsiri sahihi ya vifungu husika vya sheria na ka kanuni kuhusu mwenendo wa Bunge
hilo. Kuna sababu za kisheria za kuhoji utendaji wa Bunge Maalumu la Katiba na hasa
ikiwa kutokuwa tayari kuijadili Rasimu rasmi ya Tume ya Warioba kama msingi wa Bunge
Maalum mwezi wa Agosti, 2014 kutaendelea.
Hii ni njia isiyoridhisha tukiilinganisha
na njia ya kubadilika kwa hiari na kuomba radhi, ambayo ingeacha mwanya wazi na chanya
kuanzisha upya mjadala juu ya uundwaji wa Katiba Mpya na kufikia mwafaka na maridhiano
ya kitaifa.
Je, ni busara kuruhusu ukosefu wa muafaka katika
Bunge Maalum kuendelea?
Kuruhusu hali ya ukosefu wa muafaka ulioliteka
Bunge Maalum kuendelea, na kuwa na suluhu iliyolazimishwa na Chama Tawala kwa Watanzania,
si busara na ina hatari ya kuchochea utumiaji wa nguvu katika jamii kwa ujumla, ambao
unaweza kujitokeza katika namna mbalimbali tofauti, lakini yote yakileta madhara kwa
jamii nzima. Baadhi ya madhara ni kama yafuatayo:
Kupata kura ya
maoni ya “Hapana” katika mojawapo ya Nchi Washirika wa Muungano wa Jamhuri ya Tanzania
ni kukaribisha kuingiliwa mara kwa mara na kusikoisha katika utawala wa siku hadi
siku wa Nchi yetu.
Kujenga hali ya kutojali uongozi
wa nchi na taasisi zake, hali ambayo ni sawa na mgomo baridi wa wananchi ambao unafanya
utawala upoteze uhalali na mvuto wa kuongoza. Kutoa hongo ili kupata makubaliano juu
ya Rasimu Mbadala isiyotokana na wananchi kutaifanya Rasimu hiyo itangetange na kupeperuka
haraka na kuongeza au kuchochea hali ya wasiwasi yenye shari.
Mitafaruku katika jamii kutokana na masuala ambayo hayajapatiwa suluhu
kama umasikini, ukosefu wa ajira, ukosefu wa fursa na ukosefu wa tabia ya uadilifu
katika uongozi na utawala wa Nchi utakumbwa na mtafaruku wenye mlolongo wakutoridhika
na mchakato wa uundaji wa Katiba Mpya.
HITIMISHO Kwa kuhitimisha, tunaviomba
na kuviasa Vyama vya Siasa vyenye uwakilishi katika Bunge Maalum, hasa Chama Tawala,
kuweka upandeni maslahi ya misimamo yake, wajipambanue kwa hoja madhubuti zenye kufikiria
hasa Wananchi na Taifa. Ni kwa maslahi ya Vyama vyote vya Siasa, na hasa Chama Tawala,
kubaki na imani ya wananchi. Vinginevyo, watu watahisi wamesalitiwa na watapoteza
imani na maelewano na vyama ambavyo hadi sasa wamekuwa wakiviamini na kuvikubalii.
Kwenye uchaguzi, wanaweza hata kuvinyima kura.