2014-08-02 08:53:19

Jifungeni kibwebwe kupalilia miito mitakatifu!


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, CCEE linaendelea kufuatilia kwa umakini mkubwa myumbo wa miito ya maisha ya kipadre na kitawa Barani Ulaya sanjari na kushuka kwa idadi ya waamini wanaoshiriki katika maisha na utume wa Kanisa; yaani waamini wanaohudhuria Ibada na Liturujia mbali mbali kama sehemu ya mchakato wa maisha yao ya Kikristo. RealAudioMP3

Maaskofu wanatambua changamoto hii na ndiyo maana wameamua kuifanyia kazi katika mkutano wa wakurugenzi wa miito kutoka Barani Ulaya uliofanyika hivi karibuni Jimboni Varsavia, Poland. Ili kuzungumzia wito na maisha ya Kipadre na Kitawa, waamini wanapaswa kwanza kabisa kumtambua Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Hapa ni mwanzo wa hija ya maisha na utume wa Kipadre.

Kumbe, kuna haja kwa Kanisa kukazia majiundo yatakayowasaidia vijana kumfahamu Yesu Kristo, ili waweze kuwa tayari kujisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Majiundo ya awali na endelevu ni muhimu sana katika hatua mbali mbali za maisha ya vijana wanaonesha ari na wito wa kutaka kuwa Mapadre na Watawa.

Hata leo hii, Mwenyezi Mungu anaendelea kuwaita vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ili waweze kujisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, licha ya changamoto na vizingiti ambavyo vijana wanakabiliana navyo katika hija ya majiundo yao. Watu wengi wanaendelea kumezwa na malimwengu kiasi cha kushindwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa uwepo wa Mungu katika maisha yao.

Majiundo ya Kipadre yatoe kipaumbele cha pekee kwa Majandokasisi kumfahamu, kumpenda na hatimaye waweze kujitoa kumtumikia Yesu, Kanisa na jirani zao kwa kutambua kwamba, wito wao ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayowawajibisha.

Yesu anaendelea kuwaita vijana na wasichana kumfuasa katika maisha ya Kipadre na Kitawa, ingawa takwimu zinaonesha kwamba, hali ya miito ya maisha ya Kipadre na Kitawa Barani Ulaya inachechemea kwa kasi ya ajabu, changamoto ya kuibua mbinu na mikakati ya shughuli za kichungaji, ili kuwasaidia vijana kutambua na kuimarisha miito yao kwa kufanya maamuzi magumu kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko.

Miito inaweza kuzaliwa, kukuzwa na kuendelezwa, ikiwa kama waamini watatambua dhamana yao katika maisha na utume wa Kanisa. Waamini wajenge na kukuza moyo wa Sala, Ibada na ushiriki wa Sakramenti za Kanisa hasa Ekaristi Takatifu na Kitubio; Sakramenti zinazowaonjesha waamini huruma na upendo wa Mungu pamoja na kuwapatia nguvu ya kusonga mbele katika kumshuhudia Kristo kwa kujisadaka kwa ajili ya jirani zao.

Kuna haja kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko kwa waamini kujenga na kuimarisha urafiki na Yesu pamoja na Mapadre na Watawa wenyewe kutoa ushuhuda wenye mvuto na mashiko! Vinginevyo ni kuendelea kumpigia Mbuzi gitaa pasi na mafanikio yanayokusudiwa!








All the contents on this site are copyrighted ©.