2014-08-01 10:07:19

Vyombo vya mawasiliano ya jamii ni nyenzo ya imani na amani!


Jukwaa la Shirikisho la Wanahabari Wakatoliki Barani Afrika, UCAP, hivi karibuni limehitimisha mkutano wake uliokuwa unafanyika mjini Bamako, Mali, kwa kuongozwa na kauli mbiu "Vyombo vya mawasiliano ya jamii ni nyenzo msingi ya amani na majadiliano Barani Afrika".

Mkutano huu ulifunguliwa na Bwana Thierno Amadou Hass Dialo, Waziri wa masuala ya dini na ibada nchini Mali, aliyewataka waandishi wa habari Wakatoliki kuwa ni vyombo vya vya imani na wajumbe wa amani. Waandishi wa habari wanapaswa kueneza habari zitakazosaidia kujenga na kuimarisha umoja wa kitaifa, maendeleo na mawasiliano yanayowajibisha.

Kwa upande wake, Askofu mkuu Jean Zerbo wa Jimbo kuu la Mali anaona kwamba, ni rahisi sana kuweza kudhibiti kinzani za kisiasa, lakini kinzani hizi zinapochukua sura ya udini na ukabila, Jamii inajikuta kwamba, iko hatarini kutumbukia katika maafa makubwa. Hivyo Askofu mkuu Zerbo amewataka waandishi wa habari kutekeleza dhamana yao nyeti kwa kuwajibika barabara, kwa kuangalia matatizo na changamoto wanazokabiliana nazo.

Wajumbe wa mkutano huu wamekumbushwa kwamba, mawasiliano ya jamii ni nyenzo msingi katika kushiriki mchakato wa Uinjilishaji Mpya, ili kuwatangazia watu wa nyakati hizi Injili ya Furaha. Ni changamoto kubwa inayopania kuenzi Injili ya Uhai, uhuru wa kuabudu, haki na amani, maendeleo, mshikamano pamoja na kuwarithisha vijana wa kizazi kipya tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu.

Ili kurithisha mambo haya kuna haja kwanza kwa waandishi wenyewe wa habari kuwa ni mashahidi wa imani ili kuweza kuwashirikisha wengine ule utajiri unaobubujika kutoka katika undani wa mioyo yao! Waandishi wa habari wawe kweli ni vyombo vya kutangaza imani na huduma ya amani. Mkutano huu umehudhuriwa na wajumbe kutoka katika nchi kumi na nne za Kiafrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.