Papa atembelea makao makuu ya Wayesuit na kupata nao chakula cha mchana
Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Mtakatifu Inyasi wa
Loyola, mwanzilishi wa Shirika la Wayesuit, iliyoadhimishwa na Mama Kanisa hapo tarehe
31 Julai 2014, ametembelea Makao makuu ya Wayesuit yaliyoko mjini Roma pamoja na kupata
chakula cha mchana na Wayesuit wanaoishi hapo.
Baba Mtakatifu Francisko ameonesha
nia hii kwa mkuu wa Shirika ili kuweza kuwa pamoja na ndugu zake katika imani, katika
hali ya faragha pasi na makuu.
Taarifa inaonesha kwamba, Baba Mtakatifu Francisko
mara baada ya chakula cha mchana, ameendelea kuzungumza na Wayesuit kwenye chumba
cha mapumziko, huku wakijipatia kahawa. Wakati wa chakula cha mchana wameshiriki pia
ndugu zake Padre Paolo Dall'Oglio, Myesuit, aliyetekwa nyara mwaka mmoja uliopita
huko Syria hadi sasa hajulikani mahali alipo.
Baba Mtakatifu amebadilishana
maneno ya faraja na ndugu hawa kwa kuthamini na kutambua mchango uliotolewa na Padre
Paolo Dall'Oglio katika maisha na utume wake. Katika chakula hiki, walikuwepo pia
Wajesuit kutoka Ulaya wanaoendelea na majiundo yao kwa kushiriki katika semina maalum.