2014-08-01 12:22:09

Changamoto za maisha ya ndoa na familia!


Baba Mtakatifu Francisko kwa kusoma alama za nyakati na kutambua matatizo na changamoto zinazoendelea kuzikabili familia nyingi za Kikristo katika maisha na utume wake, ameamua kuitisha Sinodi Maalum ya Maaskofu ili kuweza kusali, kutafakari na hatimaye, kushirikishana kuhusu: hali ilivyo, matatizo na changamoto wanazokabiliana nazo katika maisha na utume wa Familia kwenye ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. RealAudioMP3

Kanisa linataka kuwaonjesha tena wanandoa umuhimu na uzuri wa maisha ya ndoa na familia kadiri ya mpango wa Mungu kwa maisha ya mwanadamu. Mama Kanisa anakumbusha kwamba, daima kuna uhusiano wa dhati kati ya Sakramenti ya Ndoa na Sakramenti nyingine za Kanisa, hususan Ekaristi Takatifu na Sakramenti ya Kitubio.

Pale ambapo wanandoa wanavunja maagano yao ya ndoa na kuamua kuoa au kuolewa tena wanajikuta wakikikabiliana na vizuizi vya sheria za Kanisa, changamoto kubwa kwa waamini wenyewe na viongozi wao wa Kanisa. Ni jambo la muhimu sana kwa mwamini kutambua hali yake na kujizuia kwenda kinyume na sheria pamoja na utaratibu uliowekwa na Mama Kanisa.

Utafiti wa kina uliofanywa Jimbo kuu la Torino, Kaskazini mwa Italia unaonesha kwamba, kuna asilimia kubwa ya Mapadre nchini Italia wasiowafahamu wanandoa walioachika na kuamua kuoana tena, ambao hawashiriki Komunio Takatifu. Hii inaonesha kwamba, kuna baadhi ya wanandoa walioachika na kuamua kuoana tena wanaoendelea kukomunika licha ya kuwa na kizuizi cha kupokea Sakramenti hii.

Baadhi ya Mapadre wamekiri kwamba, katika Parokia zao, kuna kundi la waamini wachache ambalo limeendelea kuwa aminifu kwa mafundisho, sheria na kanuni za Kanisa. Halikomuniki, lakini linaendelea kushiriki vyema katika maisha na utume wa Kanisa. Kwa wanandoa wenye vikwazo pengine wanashindwa kutambua umuhimu wa Sakramenti ya Upatanisho na Ekaristi Takatifu katika maisha yao na hivyo wanajikuta wakishiriki Mafumbo Matakatifu kwa mazoea!

Utafiti huo unaonesha kwamba, wakati mwingine, hata Mapadre wenyewe licha ya kufahamu vizuizi vya wanandoa hao, wameendelea kuwakomunisha kwa kuogopa macho na maneno ya watu ambayo yangeweza kubadilika na kuwa ni kikwazo hasa kwenye vyombo vya habari!

Wanandoa wengine, ili kuogopa makwazo katika Parokia zao, wanaamua kuhamia Parokia nyingine, wasikofahamika na hivyo wanaendelea kukomunika. Hizi ni kati ya changamoto zinazopaswa kufanyiwa kazi wakati wa Maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia. Bado kuna kundi kubwa la waamini linalopokea Ekaristi Takatifu bila ya kufanya maandalizi makini ya maisha ya kiroho kwa kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho.

Katika hali tete kama hii, Mababa wa Sinodi watakuwa na mchango mkubwa katika kuyapatia ufumbuzi, masuala haya yanayoendelea kusababisha mkanganyiko wa mawazo kuhusu Sakramenti ya Ndoa, Ekaristi Takatifu na Upatanisho.








All the contents on this site are copyrighted ©.