2014-07-31 10:28:30

Afrika ya Kusini yashikamana na wananchi wanaoteseka Mashariki ya Kati!


Baraza la Maaskofu Katoliki Afrika ya Kusini, limemwandikia barua ya mshikamano na upendo Patriaki Fuad Tawal wa Yerusalemu pamoja na Familia ya Mungu huko Mashariki ya Kati kutokana na vita inayoendelea huko Mashariki ya Kati, hali ambayo imesababisha mateso na mahangaiko makubwa kwa watu wasiokuwa na hatia. Maaskofu wanakumbuka kwa uchungu mkubwa madhulumu na nyanyaso wanazokabiliana nazo, jambo ambalo kamwe haliwezi kuvumika.

Maaskofu wanasema, mateso na mahangaiko ya wananchi wa Palestina yamefikia kiwango cha hali ya juu. Wanapenda kuungana nao kwa njia ya sala na mshikamano wa dhati, kwa kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kuongeza shinikizo litakalosaidia upatikanaji wa amani ya kudumu huko Mashariki ya Kati. Ikiwa kama Afrika ya Kusini, ilifanikiwa kukomesha utawala wa ubaguzi wa rangi, wanatumaini kwamba, mshikamano wa kimataifa unaoweza kusaidia pia kukomesha vitendo vyote vya ukosefu wa haki msingi za binadamu.

Maaskofu wanawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuwa ni mashahidi wa Injili na vyombo vya amani, ili kuweza kusitisha chuki na uhasama kati ya watu. Maaskofu wanawahakikishia sala zao katika kipindi hiki kigumu! Ujumbe huu umetiwa sahihi na Askofu mkuu Stephen Brislin, Rais wa Baraza la Maaskofu KatolikiAfrika ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.