2014-07-30 10:14:52

Mkutano mkuu wa wanafunzi vijana Wakatoliki kufanyika Libreville, Gabon


Mtandao wa Wanafunzi Wakatoliki Afrika, ulioanzishwa kunako mwaka 1987, kwa lengo la kuwaunganisha wanafunzi waliosoma katika vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu zinazomilikiwa na kuongozwa na Kanisa Katoliki Barani Afrika, kuanzia tarehe 3 hadi tarehe 7 Agosti 2014, utaadhimisha mkutano wake mkuu wa saba unaofanyika kila baada ya miaka miwili mjini Libreville, huko Gabon.

Mkutano huu unaongozwa na kauli mbiu "Ujenzi wa mtandao wa wanafunzi vijana wakatoliki ili kulinda utambulisho wa mwafrika Barani Afrika na Ulimwenguni". Lengo la mkutano huu ni kuwapatia fursa wanafunzi vijana Wakatoliki kufanya tathmini kuhusu mchango wao ndani ya Kanisa na katika ulimwengu.

Vijana hawa pia watapata fursa ya kutafakari ujumbe wa siku ya kuombea amani duniani uliotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa mwaka 2014. Ni ujumbe unaokazia udugu kama njia ya amani. Vijana wanapenda kupambanua mbinu mkakati wa mawasiliano, utakaowawezesha kutekeleza dhamana na wajibu katika maisha na utume wa Kanisa pamoja na kuanzisha makao makuu yatakayosimamia na kuratibu kazi za mtandao huu.

Maadhimisho ya mkutano huu yamegawanyika katika sehemu kuu mbili: sehemu ya kwanza itajadili kuhusu: utawala bora, demokrasia, mikakati ya kujitegemea na udhibiti wa migogoro na kinzani Barani Afrika. Sehemu ya pili itajikita zaidi katika masuala ya bajeti, uchaguzi wa viongozi wapya pamoja na kuangalia Katiba ya Mtandao huu. Mkutano unatarajiwa kuhudhuriwa na vijana kutoka katika nchi mbali mbali Barani Afrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.